Wednesday, December 24, 2014

BOZI BOZIANA ‘MZEE BENZI’ ASIYECHUJA KIMUZIKI



BOZI BOZIANA ‘MZEE BENZI’ ASIYECHUJA KIMUZIKI.

Bozi Boziana  ‘mzee Benzi’ kama anavyojulikana na wengi ni mwanamuziki ni kiongozi wa kundi  Anti Choc toka Jamhuri ya Kidemokrasi ya Kongo.

Licha ya umri wake kuwa mkubwa, awapo jukwaani huwezi kuamini macho yako unapomuona akiimba na kucheza sambamba na wanenguaji wa bendi hiyo.

Muziki wa nguli huyo huwa hauchuji kama ilivyo kwa wanamuziki wengine.

Bozi amejizolea sifa lukuki kwa kuweza kuongoza kundi hilo ambalo ni miongoni mwa bendi zinazokubalika huko Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo.

Sifa nyingine kubwa ya mwanamuziki huyo ni kwamba pamoja na utunzi na uimbaji Bozi pia ni mkung’utaji mzuri wa gita, aliyepitia katika bendi nyingi kupiga muziki katika mtindo wa soukous.

Imani iliyojengeka kwa baadhi ya wadau wa muziki ni kwamba mwanamuziki bora ni yule anayekubalika kupiga muziki katika bendi yeyote atakayokwenda.

Kama ni hivyo basi miongoni mwa hao ni Bozi Boziana ambaye aliwahi kupitia bendi nyingi zikiwamo za Bamboula de Papa Noel,  na Zaiko Langa Langa. Zingine zilikuwa za Isifi Lokole, Yoka Lokole, Langa Langa Stars na Choc Stars

Baada ya kupata uzoefu wa muda mrefu katika muziki, alihamasika kuunda bendi yake, akaweza kuanzisha bendi ya Orchestra Anti-Choc.

Wasifu wa mwanamuziki huyo unaeleza kuwa jina lake kamili anaitwa Mbenzu Ngamboni Boskill.
Alizaliwa  mwaka 1952 huko Jamhuri ya Kidemkokrasia ya Kongo.

Alianza muziki wa Afro-Pop katika  bendi ya Air Marine. Mafanikio yake katika muziki  alianza kuyaona ilipotimu mwaka 1974, alipojiunga na bendi ya Zaiko Langa Langa.

Hapo Zaiko alishirikiana na waimbaji  wengine mahiri wakati huo, wakiongozwa na mkongwe  Papa Wemba na mwezake Evoloko Jocker.

Kabla mwaka  haujatimia, waimbaji Papa Wemba na Evoloko waliondoka katika bendi hiyo ya Zaiko Langa Langa.

Kuondoka kwao kulikuwa ni changamoto kwa Bozi Boziana ambaye naye aliamua kuwafuata na wakanzisha bendi mpya ikaitwa Isifi Lokole

Kukosekana kwa uongozi madhubuti kulisababisha kutokukubaliana katika masuala mbalimbali ya msingi, miongoni yakiwemo ya kimaslahi.

Mtafaruku huo uliwafanya wanamuziki akina Papa Wemba, Boziana, Mavuela Somo na wengine kuondoka bendi ya Isifi Lokole’  wakaunda bendi nyingine mpya iliyopewa jina la Yoka Lokole.

Bozi baada ya kuona kaachwa mithiri ya mkiwa, mwaka 1977 naye akaondoka Yoka Lokole licha ya bendi hiyo kuwa maarufu kwa kipindi kifupi.

Kwa miezi michache  Boziana alishirikiana na mwanamuziki Efonge Gina, ambaye naye alikuwa katika bendi ya Zaiko Langa Langa.

Walirekodi nyimbo kadhaa kama vile Selemani iliyotungwa na Bozi na  Libanko Ya Ngai utunzi wake Gina.

Produza maarufu Kiamuangana Mateta ‘Verckys’ ambaye ni mkongwe wa muziki nchini huo mwaka 1981, aliibadilisha  bendi ya Soukous Super group  na kuita  Langa Langa Stars.

Bendi hiyo alikuwa imejaza wanamuziki waliokuwa na vipaji tofauti akina Evoloko Jocker, Dindo Yogo na  wnengine wengi.  Bozi Biziana alialikwa kujiunga vijana hao naye akaubali na kuicha  Zaiko Langa kwa mara ya pili.

Boziana alidumu kwa miaka michache hapo Langa Langa Stars kabla ya kuondoka kwenda kujiunga na bendi kubwa nchini humo  Choc Stars aliyokuwa chini Ben Nyamabo ambako alipiga hadi mwezi Novemba 1985.

Akiwa na bendi hiyo ya Choc Stars alirekodi baadhi ya nyimbo ambazo zilikuja kuwa maarufu za Sandu Kotti, Alena, Mbuta-Mutu na Retrouvailles a Paris.


Bendi ya Choc Stars ilikuwa na wanamuziki wengi wenye vipaji lukuki akina Fifi Mofude, Djo Nolo, Koffi Alibaba, Wally Ngonda, Rigo Star, mpiga gita la besi Ngouma Lokito.

Boziana aliwahi kushinda zawadi ya Kora All-African kwa album yake kuwa bora toka nchi za Afrika ya Kati.

Kwa wapenzi wa muziki hapa nchini watamkumbuka Bozi jinsi alivyoteka wapenzi katika maonesho kadhaa aliyoyafanya hapa nchini kwa ushirikiano walioonshea kati ya Bozi Boziana, Deesse Mukangi na Joly Detta walivyokuwa wakilishambulia jukwaa kwka staili ya ‘Nzawisa’ katika nyimbo za Tembe na Tembe, Palpitation na zingine nyingi zilifanya watu kuviacha viti vyao kwenda kuwatuza.

Bozi Boziana ana sauti nzuri, yakupendeza akimba huku akipokezana na timu yake ya wanadada wawili, Joly pamoja na Deesse.

Sifa nyingine za mwanamuziki huyu mzee Benzi ni kwamba muziki wake hauna mwingiliano kati ya sauti ,gitaa na synthesizer katika nyimbo zake zote. Mfano katika wimbo wa ‘Ngoyartong020’ tune tatu za mwanzo Boziboziana amemshirkisha Jolly Detta na Deesse,  na sehemu ya pili ya wimbo huo aliongeza nguvu kwa kumuongeza waimbaji na wanenguaji  Scola Miel maarufu kwa jina ‘Nzawissa’ na Betty.

Bozi alifyatua vibao vingi vilivyompa sifa nyingi ukiwemo wa La reine de Sabah, Lelo Makambo Lobi Makambo Evelyne na Fleur de Lys ambazo alimshirikisha mwimbaji wa kike Joly Delta.
Boziana aliachia wimbo mwingine akimshirikisha Deesse na Ba Bokilo.

Bozi Boziana na bendi yake bado anaendeleza muziki akiwa na bendi yake na watanzania watakumbuka kwa mara ya mwisho alikuja hapa nchini kwa mwaliko wa African Stars Entertainment Tanzania (ASET) iliyo chini ya uongozi wa Mkurugenzi Asha Baraka.

Mwisho.

LOVY LONGOMBA ALIYETOKEA KATIKA FAMILIYA YA WANAMUZIKI.



LOVY LONGOMBA ALIYETOKEA KATIKA FAMILIYA YA WANAMUZIKI.

 “Mwana wa Nyoka ni Nyoka…” usemi huu wa wahenga unajionesha wazi kwa baadhi ya familiya zilizo jaaliwa vipaji vikubwa.

Kuna familiya zilizojaaliwa kuwa za wacheza mpira wa miguu, nyavu, na michezo mingine.

Mifano halisi ni kwa wanadada wawili Wamarekani weusi, Serena na Vunus Williams, ambao ni mabingwa Kimataifa katika kucheza mpira wa Tennis. 

Hapa nchini familya ya Uvuruge ilikuwa na watoto waliokuwa na vipaji vya kutunga  nyimbo na kupiga muziki.  Ndugu hawa Jumanne, Stamili, Huluka na Maneno, walijijengea sifa tele katika muziki hapa nchini.

Familiya ya akina Kihwelu nayo ilikuwa na viaji vya kucheza mpira wa miguu, ambapo walikuwepo akina Mtwa, Jamhuri ‘Julo’  na ndugu zao wengine.
Kwa upande wa ngumi, familiya ya Matumla imerithisha kucheza mchezo wa ndondi takribani familiya nzima.

Katika makala hii ambayo itamzungumzia Familiya ya Longomba, toka Jamhuri ya Kidemokrasi ya Kongo. Vicky Longomba ndye aliye kuwa baba wa familiya ya watoto wengi waliojaaliwa vipaji vingi vya muziki.

Huyo Mzee Vicky Longomba  alikuwa mmoja kati ya wanamuziki waliokuwa waanzilishi wa bendi ya T.P.OK. Jazz iliyokuwa ikiongozwa na Franco Luanzo Makiadi.

Pia ikumbukwe kwamba  Vicky ndiye  aliyekuwa  mwanzilishi wa bendi ya Lovy du Zaire, iliyotamba kwa muziki nchini Kongo mwaka 1971.

Kwa kuwa familiya hiyo ina wanamuziki wengi leo katika makala hii itamzungumzia mmoja wa watoto wake Lovy Longomba.

Wasifu wa mwanamuziki huyo unaelezea kwamba alianza muziki katika bendi ya Orchestra Macchi mwaka 1976, akiwa na mwimbaji mwenzake Dindo Yogo.

Aidha walikishirikiana na mpiga gita Nseka Huit, waliondoka katika bendi ya Macchi na wakaunda bendi yao ya  Etumba na Ngwaka wakiwa na waimbaji wengine akina Lofanga, Gaby Yau-Yau na Mukolo, aliyekuwa akiimba sauti ya kwanza.

Wanamuziki wengine waliokuwepo katika bendi hiyo ni pamoja na Huit Kilos, ambaye baadaye alikwenda kuwa nyota katika bendi ya Afrisa International ya Tabu Ley Rochereau.

Mwanamziki Ricardo aliondoka na kwenda katika bendi ya Lemvo in Makina Loca, iliyo na makao yake huko  Los Angeles, Marekani.

Inaelezwa kwamba Lovy Longomba alikuwa mtunzi na mwimbaji mahiri. Alikuwa kaka wa wanamuziki machachari Awilo Longomba.

Awilo kabla ya kuanza kutunga na kuimba, alikuwa mcharazaji hodari wa drums katika bendi mbalimbali nchini humo. 

Lovy naye pia alikuwa baba wa familiya yenye watoto wanamuziki akiwemo binti yake aliyerithi uimbaji, Elly Longomba na mapacha Christian na Lovy ambao wote ni nyota katika muziki  wa Hip-hop, wakimiliki Kampuni ya ‘Longambas’ huko Nairobi, nchini Kenya.

Baadaye  Agosti 1978, Lovy aliicha bendi ya Orchestra Macchi, na kuamua kuondoka  Kinshasa. Alitiga katika jiji la Nairobi nchini Kenya ambako alijiunga katika bendi ya  Les Kinois.
Kwa kuwa ‘Kiu’ chake hakikuwa kimekidhiwa, Lovy alidumu kwa miezi mitatu pekee,
akatimkia katika bendi ya Boma Liwanza.

“Maisha ni kutafuta” mbio za kutafuta maisha zikaendelea. Baada ya miezi sita Lovy alitimka na kuiacha Boma Liwanza, akajiunga na bendi ya Super Mazembe iliyokuwa ikiongozwa na  Mutonkole Longwa Didos.
Akiwa katika bendi hiyo alionesha uhodari wa kutumia sauti yake ilivyokuwa nyembemba na nyororo, ambayo ndiyo iliyopelekea kwa yeye kupachikwa jina bandia la ‘Ya Mama’. Sababu kubwa ni kwamba alikuwa na uwezo wa kuimba sauti ya juu ambayo alipashwa aimbe mwanamke.

Katika bendi hiyo alikutana na  wanamuziki wenzake mahiri akina Joseph Okello Songa, Kasongo wa Kanema, Musa Olokwiso Mandala na Fataki Lokassa ‘Masumbuko ya duniya’ aliyekuwa ametokea katika bendi ya Les Noirs.

Baadhi ya nyimbo alizoachia katika bendi Super Mazembe ni pamoja na ‘Lovy’, ‘Yo mabe’, ‘Ndeko’, ‘Nanga’, ‘Mokano’ na ‘Elena’.
Sauti yake nyororo mara nyingi husikika katika baadhi ya nyimbo za bendi hiyo, akibwagiza akitamka “Vuta sigara SM, maana yake Super Mazembe…”

Hata hivyo umahiri wa kutunga na kuimba katika bendi hiyo, ilisababisha kuhitajika takribani na kila bendi.
Kwa mara nyingine tena Lovy aliondoka Super Mazembe mwaka 1981 akaenda kuimba katika bendi ya Shika Shika, iliyokuwa ikiongoza na Jimmy Monimambo, kwa miaka miwili.

Ndoto zake za kumiliki bendi yake zilitimia baada ya yeye na wanamuziki wenzake alipounda bendi yake Super Lovy ikiwa na Nembo ya AIT.

Lakini kwa kile alichokieleza ni kuepuka mkanganyiko na mvutano aliamua kutumia jina Bana Likasi  wakati aliporekodi  katika  Kampuni ya Audio Productions Ltd.


Akiwa na bendi hiyo, Lovy alipachikwa jina bandia la ‘Ya Mama’  kwa kile kilichoelezwa  kwamba alikuwa anauwezo mkubwa wa kuimba sauti  nyembamba ambayo ingelistahili kuimbwa na mwanamke.
Mnamo mwaka 1988 Lovy aliingia Tanzania katika jiji la Dar es Salaam na akapigia katika bendi Orchestra Afriso Ngoma.
Maisha ya nguli huyo yalikatishwa ghafla katika ajali iliyopelekea kufariki dunia nchini Tanzania mwaka 1996.
Mungu aiweke roho yake pahala pema peponi, amina.

Mwisho.
Mwandishi wa makala hii anapatikana kwa namba:
0784331200, 0767331200 na 0713331200.



BURIANI ISSA NUNDU

 BURIANI ISSA NUNDU.
“Kwa vyovyote vile kifo hakizoweleki” usemi huu ulitamkwa na mzee Kassim Mapili katika moja ya misiba jijini Dar es Salaam.

Kauli hiyo nikaiweka kichwani na hivi karibuni wapenzi mashabiki wa muziki wa dansi wamempoteza mwanamuziki Issa Nundu.

Nundu alikuwa mtunzi na mwimbaji mashuhuri aliyepiga muziki katika bendi tofauti kwake Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo na hapa nchini.

Nundu aliugua maradhi yaliyopelekea kulazwa kwa kipindi kifupi katika hospitali ya KCMC ya mjini Moshi mkoani Kilimanjaro, ambako Oktoba 25, 2014 aliiga dunia.

Akizungumza kwa simu toka Stockholm nchini Sweden,  mwanamuziki Dekula Kahanga ‘Vumbi’
alimuelezea Nundu kuwa alizaliwa Julai  23, 1954 huko Uvira, Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo.

kiwa Uvira Nundu alifanya kazi katika hospitali ya Uvira kama Mfamasia. Akiwa katika hospitali hiyo alikuwa akifanya kazi asubuhi hadi mchana, ambapo usiku alikuwa akienda kupiga muziki katika bendi ya Bavy National. 

Issa mungu  alimjaalia sauti nyororo iliyopelekea kupendwa hususani kwa wapenzi na mashabiki wa bendi ya Bavy National.

Alikuwa na uwezo wa kukariri kisha kuimba nyimbo za wanamuziki wakongwe mbalimbali zikiwemo za akina Dk. Nico Kasanda wa Afrcan Jazz.

Dekula akizungumzia wasifu wa Nundu amesema kwamba aliwahi kufanya naye kazi katika bendi mbili za Bavy National mjini Uvira DRC mwaka 1981 hadi 1983.
Nundu aliondoka Uvira huko Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo kuja Tanzania akifuatana na mtunzi na mwimbaji Kyanga Songa.

Walikutana tena katika bendi ya Maquis du Zaire mwaka1986, ambako anakiri kuwa Nundu alimpokea vizuri hadi alipoanza  na mipango ya kuhamia MK. Group 1990.

Baba yake Issa Nundu alikuwa  Chifu wa kijiji cha Nundu katika Wilaya ya Fizi Kivu, Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo. Ndiyo sababu hata alipotuwa hapa Tanzania, alitumia hadhi na kujiita ‘mtoto wa mfalme’ Prince Jaques Nundu.

Prince Nundu alipokuwa katika jiji la Dar e Salaam, aliwahi kupiga muziki katika bendi za Orchestra Makassy, Orchestra Super Matimila,  Maquis du  Zaire, MK. Group, Bana Maquis,  Super Kamanyola ya jijini Mwanza na La Capitale ‘Wazee Sugu’ inayoongozwa na Kikumbi Mwanza Mpango ‘King Kiki’
Prince Nundu alipokuwa katika bendi ya Makassy alikutana na waimbaji mahiri akiwemo Mbombo wa Mbomboka, Mzee Makassy na Maliki Star na wengine weingi.

Alipojiunga na bendi ya Maquis du Zaire wakati huo ikipiga katika ukumbi wa White House Ubungo, alikutana na miamba ya uimbaji akina Mutombo Lufungula ‘Audax’, Mbuya Makonga ‘Adios’ Tshimanga Assosa,  Mukumbule Lolembo ‘Parashi’, Kabeya Badu, Kalala Mbwebwe, mapacha Kassalo Kyanga na  Kyanga Songa.

Wengine walikuwa  Kiniki Kieto, Abubakar Kasongo Mpinda ‘Clayton’, Mbombo wa Mbomboka, Kikumbi Mwanza Mpango ‘King Kiki’, Tshimanga Kalala Assosa, Masiya Radi ‘Dikuba kuba’, Rahma Shaari, Anna Mwaole na  Mary Mwanjelwa.

Aliwahi kuimba wimbo uliojulikana kwa jina la ‘Sikutegemea’ambao aliimba peke yake kwa sauti yenye simanzi tele. 

Alipokwenda katika bendi ya MK. Group iliyokuwa ikipiga muziki katika hoteli ya New Afrika, Nundu alikutana na waimbaji akiwemo kiongozi wa bendi hiyo Aboubakar Kasongo Mpinda ‘Clyton’ Kapaya Vivi na wengine wengi.

Nundu alijiunga na bendi ya Bana Maquis anayoongozwa na Tshimanga Kalala Assosa, huko akakutana na waimbaji akiwemo Assosa, Anna Mwaole na Aboubakar Kasongo Mpinda ‘Clayton’
Nundu alikuwa mtafutaji hivyo alichepika katika jiji la Mwanza ‘Rocky City’ akajiunga na bendi ya Super Kamanyola. Aliimba kwa kushirikiana na  mtunzi na mwimbaji mahiri Mukumbule Lolembo ‘Parashi’ na Anna Mwaole. 

Aidha ‘Vumbi’ alitaja moja ya tungo zake ni wimbo wa Marusu ambao naye alishiriki kupiga gita ka solo waliporekodi katika studio za Redio Tanzania Dar es Salaam (RTD) mwaka 1989.

Hadi mauti yalipomfika alikuwa mtunzi na mwimbaji katika bendi ya La Capitale.