Monday, April 14, 2014

MZEE KASSIM MAPILI




MAPILI  GWIJI  ALlYETUMIA MAISHA YAKE YOTE  KATIKA MUZIKI.

Machi, 2013.

MZEE KASSIM  MAPILI  ni mwanamuziki mkongwe aliyeanza tasnia hiyo kabla ya nchi yetu ya Tanganyika, wakati huo haijapata Uhuru.
Mzee Mapili ni mwenye vipaji vingi vya kutunga, kuimba nyimbo za muziki wa dansi na kupiga gita. Pamoja na umri wake kumtupa, Mapili ni ‘mfua uji’ wakati wote  wala  haoneshi  dalili za ‘kuchoka’ kama Wazee wengine wenye umri kama wake.
Mwaka huu wa 2013, Mapili  ametimiza miaka 76 ya  kuzaliwa kwake, bado ni  mwenye nguvu, Afya njema  na kumbukumbu nyingi zilizojaa kichwani mwake.
Mzee Mapili amekula chumvi nyingi ingawaje ukikutana naye mitaani,  unaweza kumdhania kuwa  ni ‘Mzee kijana’  kwa jinsi anavyojichanganya katika maongezi na watu wa rika na jinsia tofauti
Mzee Kassim Mapili ameeleza kwamba amevuka mito, mabonde na kuparamia milima iliyoshindikana katika kuyatafuta maisha. Na amesisitaza kwamba hatokata tamaa kuendelea  kutafuta mafanikio hadi ifikapo kipindi atakapoishiwa nguvu.

.
Akisimulia historia ya maisha yake, Mzee Mapili amesema kwamba alizaliwa katika kijiji cha Lipuyu kilichopo Tarafa ya Lionya, Wilaya Nachingwea mkoani Lindi mwaka 1937.
Alipata elimu ya msingi sambamba na ya Koraan, akiwa kijijini kwake Lipuyu mkoani Lindi. Anasema akiwa madrasa alikuwa mahiri wa kughani  kaswida katika  Madrasa yake. Hata mapenzi yake ya kuimba nyimbo  aliyapata kupitia Madrasa hiyo.
Ni mwanamuziki mzoefu mwenye uwezo mkubwa wa kuimba na kupiga gita. Anasema  alianza kujifunza kupiga muziki wakati nchi yetu ikiwa bado inatawaliwa na Ukoloni wa Waigereza.
Jina la Kassim Mapili likaanza kusikika katika ulimwengu wa muziki mara tu alipojiunga katika bendi ya White Jazz iliyokuwepo mjini Lindi mwaka 1958.
Sifa zake za kupiga muziki zikazagaa sehemu mbalimbali hadi mikoa ya jirani. Hakuchuka muda mrefu katika bendi hiyo,  mwaka uliofuatia wa 1959  akahama na kujiunga na bendi ya Mtwara Jazz wakati huo.
Bendi ya Holulu ya mjini Mtwara, nayo ikaona ni bora inyakue ‘kifaa’ hicho. Mapili akashawishika na maslahi aliyo ahidiwa, ndipo alipoamua kujiunga katika bendi yao mwaka 1962.
Kwa kuwa nchi yetu ya Tanganyika wakati huo  ilikuwa tayari
imekwisha pata Uhuru, Chama TANU kiliazisha vikundi vya  Vijana kukitangaza chama hicho.
Hivyo mwaka 1963,  Mzee Mapili akaoneka anafaa kusaidia kufanya kazi hiyo, akachukuliwa kwenda katika bendi ya Jamhuri Jazz ambayo ilikuwa ya vijana wa TANU (TANU Youth League) ya Lindi.
Baada ya kufanya kazi nzuri hapo Lindi, akateuliwa kuwa muasisi wa bendi nyingine ya Vijana wa TANU (TANU Youth League) huko Tunduru,  mkoani Ruvuma mwaka 1964.
Katika kutafuta maslahi murua wakati huo, alilazimika  kwenda kujiunga na bendi ya Luck Star mwaka 1965,  iliyokuwa na makazi yake Kilwa Masoko mkoani Lindi.
‘Kizuri hupendwa popote’ Kassim hakukaa sana na Luck Star, mwaka huohuo alisakwa ‘kwa udi na uvumba’ na bendi ya Kilwa Jazz iliyokuwa ikiongozwa na Ahmed Kipande, akajiunga nayo.
Jeshi la Kujenga Taifa (JKT) lilianzisha bendi mbili za muziki wa dansi za JKT ‘Kimbunga Stereo’ na JKT ‘Kimulimuli’. Kwa kuwa sifa za  Mzee Mapili zilikuwa zimezagaa kupitia wa muziki hapa nchini,  Jeshi hilo lilimchukuwa kwenda kuwa muasisi wa bendi ya JKT Mgulani, jijini Dar es Salaam mwaka 1965.
Ushindani wa bendi katika Majeshi, ukaaza. Jeshi la Polisi nalo likamhitaji ajiunge nalo. Alikubali kwenda kuasisi bendi yao ya Polisi Jazz  baada ya kupata ajira tarehe 15, Desemba 1965. Polisi Jazz  ilikuwa ikipiga muziki wake katika ukumbi wa Polisi Barracks, jijini Dar es Salaam.
 Akiwa ‘Afande’ Mzee Kassim Mapili aliteuliwa kuwa mwalimu wa bendi ya  Wanawake ikijulikana kama Woman Jazz Band Desemba 23,1965.
Bendi hiyo ilikuwa ikimilikiwa na Umoja wa Vijana TANU (TANU Youth League) ambapo alisafiri na bendi hiyo kwenda nchini Kenya, kwenye sherehe za siku ya Kenyata.(Kenyata day) Kenyata alikuwa rais wa kwanza wa nchi ya Kenya.
Mzee Kassim Mapili alipata pigo kubwa Mei 1966, baada ya kuondokewa na baba yake mzazi Mzee Said Amri Makolela, aliyeuawa wakati akipambana  na Nyati porini. Anamshukuru mungu kwani mama yake mzazi Bi. Ajena Mussa Mtikita, bado yu hai.
Baada ya kuvunjika kwa bendi ya Woman Jazz  mwaka 1974, ndiyo ikwa mwanzo wa kuanzishwa kwa bendi ya Vijana Jazz  baada ya kuwakusanya vijana wa wakati huo akina Hemed Maneti,  Hassan Dalali, Manitu Mussa, Hamza Kalala ‘Komandoo’ Chakupele,  Abdallah Kwesa , Agrey Ndumbaro na wengine wengi.
Kassim Mapili alistaafu toka jeshi la Polisi  Mei 05, 1981 akiwa na cheo cha Sajenti. Mara baada ya kustaafu mwishoni mwa mwaka 1981, alijiunga na bendi ya Tanzania Stars Ushirika Jazz.
Kwa kipindi kirefu Mzee Mapili amekuwa  akiitwa kuhudhuria semina nyingi. Mwaka 1982,  alishiriki katika semina ya wanamuziki iliyofanyika mjini Bagamoyo. Katika semina hiyo ilipelekea kuundwa kwa Chama cha Muziki wa Dansi Tanzania (CHAMUDATA), naye akachaguliwa kuwa mwenyekiti wa kwanza wa chama hicho.
Kila panapofanyika jambo la manufaa katika muziki hapa nchini, Mzee Mapili amekuwa akishirikishwa kikamilifu. Amekuwa akitoa michango ya mawazo yenye busara katika tasnia ya muziki  kwa nyakati tofauti.
Busara zake zilipelekea mwaka 1986 kuchaguliwa kuwa mmoja wa washiriki katika uundwaji wa kundi la wanamuziki 57, lililoitwa Tanzania All Stars.
Mwaka huohuo alishiriki katika tamasha la utoaji  wa zawadi kwa Wasanii wakongwe, akiwemo Mzee Morris Nyunyusa, Mzee Makongoro, Mzee Mwinamira, Mbaraka Mwinshehe na wengine.
Kassim Mapili alikuwa muasisi katika shindano la nyimbo kumi bora za wanamuziki wa dansi (Top Ten Show) mwaka 1988, akiwa kama Mwenyekiti wa CHAMUDATA.
Mzee Mapili akiwa kama Baba, aliwakumbuka watoto wa mitaani wanaosumbuka katika kutafuta maisha. Alianzisha bendi ya watoto  wa umri wa miaka 16,  ambao baadaye walifanya onesho kamambe,  sambamba na siku ambayo watoto wa Afrika Kusini waliteswa huko Soweto.
Mapili mwaka 1993, alikuwa mstari wa mbele wa uanzishwaji wa bendi ya Wazee ya Shikamoo Jazz. Bendi hiyo bado ipo ikiongozwa na Mzee Salumu Zahoro.
Hekima na busara za Mzee  huyu,  zilipelekea mwaka 1974, kuteuliwa kuwa mlezi wa bendi ya Super Matimila.
‘Aliyena nacho huongezewa’ usemi huu ulijiri kwa Mzee Kassimu Mapili,  ambaye Nyota yake aliendelea kung’ara, aliteuliwa kuwa mkufunzi wa bendi ya Gold All Stars mwaka 1977.
Mzee Mapili hakuwa mchoyo wa kugawa ujuzi alionao, kwani alishiriki kikamilifu katika uundwaji upya wa bendi ya Super Volcano, akiwa na binti ya Mbaraka Mwinshehe, Taji.
Kama nilivyotangulia kukujuza kwamba  Mzee Mapili anaonekana si mtu wa kuchoka kiafya, siri yake alilidokeza hivi. “Nakula chakula vizuri,  ninafanya mazoezi ya viungo kila siku, Sigara, Pombe na starehe zisizokuwa za lazima, kwangu  ni  mwiko…”  Mzee Mapili anafafanua siri ya mafanikio ya afya yake kuwa imara hadi leo.
Pamoja na umri wake kuwa mkubwa, anasema bado  hajafikia wakati wa kuwa tegemezi kwa watoto wake. Anamiliki bendi ya Orchestra Mapili Jazz ambayo bado haijafahamika kwa kiasi kikubwa kwa baadhi ya washabiki wake.
“Bendi yangu huwa inawasisimua mno wapenzi wa muziki wa zamani kwa kuwapigia nyimbo za zamani kwa maombi yao maalum…”  anasema Mapili.
Kassim alienda mbali zaidi akijigamba kwamba wakati akipiga gita, huimba  kufanya ‘shoo’ mwenyewe  akiwakumbusha wazee wenzake mitindo yao ya  zamani ya Twist, Bumping, Charanga, Chacha na Pachanga.

“Nikianza kucheza Twist, juu… juu… chinii… chinii… juu… chiniii,  watu ukumbini huzizima na kunizunguka wakinipongeza wangine wakisema  “Wazee dawa…”  Mapili anatamka kwa kijiamini huku akionesha jinsi ya kucheza mtindo huo.
“Ninauheshimu sana muziki kwani ndiyo ulionilea hadi sasa. “Nimekulia na kuzeeka nikiwa katika muziki, sijawahi kufanya kazi nyigine tofauti na muziki katika maisha yangu yote. Hata nilipopata ajira katika Jeshi la Polisi, nilikuwa akifanya kazi ya muziki…” Anasema Mapili.
Kassim Mapili ni baba wa familiya ya mke na watoto watatu, aliowataja kwa majina ya Kuruthum, Said na Hassan. Kati yao hakuna hata mmoja aliyefuata nyao zake za muziki.
Mapili amekuwa mstari wa mbele katika shughuli takriban zote za kifamiliya za wasanii na wanamuziki wenzake hapa nchini. Huwa habagui kwamba ni Mtanzania ama vinginevyo. Mfano halisi wiki iliyopita  kabla ya kifo cha mwanamuziki Kabeya Budu wa bendi ya Le Capitale, Mapili alikuwa mstari wa mbele kwenda  kumjulia hali  akiwa hospitalini. Pia alishiriki kikamilifu katika mazishi ya mwanamuziki huyo Kabeya Badu, aliyefariki tarehe 06 Machi,  2013 katika hospitali ya Muhimbili kwa maradhi ya figo. Badu alikuwa raia wa  Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo DRC).

Mzee Kassim Mapili amemalizia kwa kuwasihi wanamuziki hususani vijana, kujifunza kupiga ala za muziki, ili wafikie malengo yao ya kuwa wanamuziki watakao kubalika kimataifa. Aidha amewataka kuzingatia heshima na upendo miongoni mwao.


Mwisho.


BOZI BOZIANA ' MZEE BENZI'



BOZI BOZIANA NA ANTI-CHOC



Aprill 15,2014.

Bozi Boziana au ‘Mzee Benzi’ kama anavyojulikana na wengi ni mwanamuziki anayeongoza kundi zima la Anti Choc toka Jamhuri ya Kidemokrasi ya Kongo.
Jina lake kamili anaitwa Mbenzu Ngamboni Boskill ambaye alizaliwa  mwaka 1952 huko Jamhuri ya Kidemkokrasia ya Kongo.
Pamoja na utunzi na uimbaji Bozi pia ni mkung’utaji mzuri wa gita aliyepiga katika bendi nyingi kubwa nchini mwao zinazopiga katika mtindo wa soukous.
Baadaye akaunda bendi yake Orchestra Anti-Choc.
Mzee Benzi aliazia muziki wa Afro-Pop katika  bendi ya Air Marine lakini alianza kuyaona mafanikio ya kazi zake ilipotimu mwaka 1974 alipojiunga na bendi ya Zaiko Langa Langa. Zaiko LangaLanga ilikuwa na waimbaji  mashuhuri wakati huo  wakiongozwa na mkongwe  Papa Wemba na mwezake Evoloko Jocker.
Lakini haikuzidi mwaka , Papa Wemba na Evoloko waliondoka Zaiko Langa Langa na Bozi Boziana aliwafuata  kwenda kuanzisha bendi mpya ikaitwa Isifi Lokole.
Kutokukubaliana katika maswala mbalimbali ya msingi kulimfanya wanamuziki Papa Wemba, Boziana, Mavuela Somo na wengine kuondoka bendi ya Isifi Lokole na wakaunda bendi mpya iliyopewa jina la Yoka Lokole.
Yoka Lokole ilipata  mafanikio makubwa mwaka 1976  lakini mwinshoni mwa mwaka huohuo Papa Wemba aliicha bendi hiyo na akaenda kuanzisha bendi ya Viva la Musica.
Bozi Boziana naye mwaka 1977 akaondoka Yoka Lokole licha ya bendi hiyo kuwa maarufu kwa kipindi kifupi.
Kwa miezi michache  Boziana alishirikiana na mwanamuziki Efonge Gina, ambaye naye alikuwa katika bendi ya Zaiko Langa Langa. Walirekodi nyimbo kadhaa kama vile Selemani iliyotungwa na Bozi na  Libanko Ya Ngai utunzi wake Gina.
Produza  Verckys Kiamuangana mwaka 1981  aliibadilisha  bendi ya Soukous super group  na kuita  Langa Langa Stars ikiwa imesheheni vipaji vya wanamuziki kaiwemo Evoloko Jocker, Dindo Yogo na  wnengine wengi.  Bozi Biziana aliakwa kujiunga vijana hao naye akaubali na kuicha  Zaiko Langa kwa mara ya pili.
 Langa Langa Stars ilidumu kwa miaka michache iliyofuatia kabla na Boziana naye akaondoka kwenda kujiunga na bendi kubwa nchini humo  Choc Stars aliyokuwa chini Ben Nyamabo ambako alipiga hadi mwezi Novemba 1985.
Akiwa na bendi hiyo ya Choc Stars Boziana alirekodi baadhi ya nyimbo ambazo zilikuja kuwa maarufu za Sandu Kotti, Alena, Mbuta-Mutu na Retrouvailles a Paris.
Anti –Choc ilikuwa na wanamuziki wengi wenye vipaji lukuki wakiwemo akina Fifi Mofude, Djo Nolo, Koffi Alibaba, Wally Ngonda, Rigo Star, Ngouma Lokito, Deesse Mukangi, Marthe Lamugenia, Ngimbi Yespe na Maoussi Solange.
Mpiga gita wa kwanza katika bendi hiyo alikuwa Matou Samuel ambaye  kwa sasa anaimba muziki wa Injili  na nafasi yake ilishikwa na Dodoly ambaye kabla ya kujiunga humo alitokea katika bendi ya mwanamuziki Lita Bembo ya Orchestre Stukas.
Dodoly alipachikwa jina bandia la ‘The sewing machine’ kwa umahiri wake wa kutumia vidole vyake kucharaza nyuzi  kwa kasi kubwa.
Tokea miaka ya 1980  Boziana aliendelea katika bendi yake ya Anti-Choc ikiwa ni pamoja na kurekodi nyimbo  akishirikiana na wanamuziki wengine mahiri.
Boziana aliwahi kushinda zawadi ya Kora All-African kwa album yake kuwa bora toka nchi za Afrika ya Kati.
Kwa wapenzi wa muziki hapa nchini watamkumbuka Bozi jinsi alivyoteka wapenzi katika maonesho kadhaa aliyoyafanya hapa nchini kwa ushirikiano walioonshea kati ya Bozi Boziana, Deesse Mukangi na Joly Detta walivyokuwa wakilishambulia jukwaa kwka staili ya ‘Nzawisa’ katika nyimbo za Tembe na Tembe, Palpitation na zingine nyingi zilifanya watu kuviacha viti vyao kwenda kuwatuza.
Bozi Boziana ana sauti nzuri, yakupendeza akimba huku akipokezana na timu yake ya wanadada wawili, Joly pamoja na Deesse.
Sifa nyingine za mwanamuziki huyu mzee Benzi ni kwamba muziki wake hauna mwingiliano kati ya sauti ,gitaa na synthesizer katika nyimbo zake zote. Mfano katika wimbo wa ‘Ngoyartong020’ tune tatu za mwanzo Boziboziana amemshirkisha Jolly Detta na Deesse,  na sehemu ya pili ya wimbo huo aliongeza nguvu kwa kumuongeza waimbaji na wanenguaji  Scola Miel maarufu kwa jina ‘Nzawissa’ na Betty. Bozi alifyatua vibao vingi vilivyompa sifa nyingi ukiwemo wa La reine de Sabah, Lelo Makambo Lobi Makambo Evelyne na Fleur de Lys ambazo alimshirikisha mwimbaji wa kike Joly Delta.
Boziana aliachia wimbo mwingine akimshirikisha Deesse na Ba Bokilo.
Bozi Boziana na bendi yake bado anaendeleza muziki akiwa na bendi yake na watanzania watakumbuka kwa mara ya mwisho alikuja hapa nchini kwa mwaliko wa African Stars Entertainment Tanzania (ASET) iliyo chini ya uongozi wa Mkurugenzi Asha Baraka.

Mwisho.


AHMED KIPANDE NA KILWA JAZZ



AHMED KIPANDE NA KILWA JAZZ.

AHMEDI  KIPANDE ni mwanamuziki nguli aliyeshiriki kikamilifu katika uhamasishaji wa maendeleo na kupigani Uhuru wa Tanganyika akiwa na bendi yake ya Kilwa Jazz.

Kilwa Jazz ilishiriki kikamilifu siku Tanganyika inapata Uhuru Decemba 09, 1961 kwa kimba wimbo wa kusifia nchi yetu kupata Uhuru toka wa Wakoloni.

Chini ya uongozi wa Ahmedi Kipande,  Kilwa Jazz ilishiriki kikamilifu kutoa burudani wakati mikakati ya kufanya Mapinduzi ya Zanzibar kwenye meneo ya makao makuu ya bendi hiyo jijini Dar es Salaam mwaka 1964.

Ahmedi Kipande na bendi yake waliteuliwa na serikali ya Tanganyika kwenda kushiriki sherehe za Uhuru wa nchi za Malawi na Uganda.

Historia ya mwanamuziki huyu iliyotolewa na mwanawe wa mwisho Kipande Ahmed, ameeleza kwamba jina kamili la  baba yake alikuwa ikiitwa Ahmed Mohammed Kipande,  aliyezaliwa mwaka 1937 huko Kilwa Kivinje mkoani Lindi.

Miaka michache baada ya kifo cha mama yake Ahmed Kipande alifuatana na Baba yake kuja Dar es Salaam na akaanza masomo katika shule ya Uhuru Wavulana ilikuwa maeneo ya Kariakoo, Dar es Salaam.

Katikati ya miaka ya 1950 Kipande alianza kupiga muziki akitumia ala iitwayo Violin, katika bendi ya Tanganyika Jazz iliyokuwa ikiongozwa na Zimbe Kidosi. Bendi hiyo ilikuwa  na makao makuu yake katika mtaa wa New Street ambao hivi sasa unaitwa mtaa wa Lumumba.
Wanamuziki wa miaka hiyo walianzisha bendi wakizipa majina ya maeneo yale  wanakotoka, hivyo waanzilishi wa Rufiji Jazz walitoka Rufiji, na ndivyo ilivyokuwa kwa Kilwa Jazz, Ulanga jazz na kadhalika.
Ahmed Kipande aliyekuwa ametoka Kilwa Kivinje mkoani Lindi nae akishirikiana na mwanamuziki mwenzake aliyetajwa kwa jina moja la Shamte nao wakaamua kuanzisha bendi ya watu kutoka Kusini ya Kilwa Jazz mwaka 1958.

Kilwa Jazz ikaanza kujizolea umaarufu kwa kutunga na kuimba nyimbo mbali mbali zikiwemo za siasa, mapenzi na za uhamasishaji kupata Uhuru wa Tanganyika.
Aliunga na kuimba wimbo wa ‘TANU yajenga nchi’, nchi yetu’  ‘enyi Vijana tujenga yetu Doli na ‘It can be done, play your party’
Zingine zilikuwa za ‘Roza waniuwa uwa’, ‘Nipate lau nafasi’, ‘Nacheka cheka Kilwa leo’ na ule wa  Maneno hayafai’

Wimbo wa Nacheka cheka ulitungwa na Ahmed Kipande baada ya kukopi wimbo wa  Tabu Ley na John Bokelo wa ‘Mokolo nokokufa’ halikadhalika nyimbo za Nacheka cheka Kilwa leo na Maneno hayafai ambazo walizikopi na kupesti toka wimbo wa Course au Povouir wa T.P.OK. Jazz.

Mwaka 1973 Kilwa jazz ilialikwa na kutumbuiza kabla ya onyesho la gwiji la muziki wa dansi, Franco Makiandi na bendi ya T.P.OK. Jazz  iliyefanya onyesho kwenye Uwanja wa taifa jijini Dar es Salaam.

Luambo Makiadi baada ya kuzisikiliza nyimbo hizo alimfuata Ahmed Kipande na kumpongeza kwa umahiri wake mkubwa wa ‘kokopi na kupesti’ pasipo kukosea.

Akimsifia baba yake Kipande Ahmed alisema kwamba mwaka 1961 siku Tanganyika inapewa Uhuru toka kwa Wakoloni, bendi ya Kilwa Jazz ilikuwa Uwanja wa taifa ikiporomosha muziki ambapo ilitoka na wimbo wa  kumshukuru mungu kwa kupata Uhuru.
Mtoto huyo wa marehemu Ahmed, aliimba mistari michache ya wimbo huo “ Ewe mola tunakuomba uibariki Tanganyika yetu na jirani  zetu, Uhuru tumepata lakini Nyoyo zina sikitika wenzetu wanateseka  Wakoloni wa mewashika…”
Bendi ya Kilwa Jazz ilikuwa na makao makuu yake katika kona ya mitaa ya Muhoro na Jangwani ambako siku moja ilipiga muziki nje ya Ofisi yao na kuwashangaza watu kuona bendi ikipiga muziki mchana. Lakini ilikuwa mipango kamambe ikipangwa maeneo hayo kwa viongozi wanamapinduzi siku chache kabla ya mapinduzi ya Zanzibar viongozi walikuwa wakipanga mikakati ya mapinduzi yaliyouondoa utawala wa Kisultani mwaka 1964 huko Zanzibar. Bendi ya Kilwa Jazz baadaye haikuelewa na jamii. Wengine wakafika mbali zaidi wakizusha maneno kwamba ni bendi ya serikali ‘eti’ ilikuwa ikialikwa kutoa burudani katika sherehe nyingi za kitaifa.
Kilwa jazz pia ilialikwa kutoa burudani katika sherehe za ndoa ya mmoja wa mawaziri wa serikali ya Tanganyika wakati huo, Oscar Kambona.

Ahmed  Kipande katika sherehe hiyo alionesha kipaji chake kwamba si cha kubahatisha. Alitunga wimbo wa papo kwa papo wa kuwasifia wanandoa hao Oscar Kambona na mkewe.
Yaelezwa kwamba Kambona aliinuka toka kwenye kiti cha maharusi na  kwenda kumkumbatika Kipande kisha akamtunza kwa pesa. 
Ni miaka 27 sasa tangu Ahmedi Mohammed Kipande afariki dunia  Aprili 27, 1987 baada ya kusumbuliwa na ugonjwa wa kiharusi kwa kipindi kirefu. Alizikwa kwenye  makaburi ya Tandika Maguruwe, mkoani Dar es Salaam  Aprili 28,1987.

Mugu ailaze roho ya marehemu Ahmedi  Kipande  pahala pema peponi,  Amen.  


JABARI LA MUZIKI MARIJANI RAJABU


 JABARI LA MUZIKI  MARIJANI RAJABU
APRILI 15,2014.

MARIJANI RAJABU KWELI HATUNAYE TENA HAPA DUNIANI LAKINI KAMWE WADAU NA WAPENZI WA MUZIKI WA DANSI HAPA NCHINI HAWATAMSAHAU.
ALIKUWA MMOJA MIONGONI MWA WANAMUZIKI WALIOTOA MCHANGO MKUBWA WA MAENDELEO YA NCHI KUPITIA TUNGO ZA NYIMBO ZAKE MARIDHAWA  ZILIZOKUWA ZIKIENDANA NA WAKATI.
MARIJANI MWEZI MACHI 23, 2014, ALITIMIZA MIAKA 18 TOKA KIFO CHAKE. NGULI HUYO ALIFARIKI MACHI 23, 1995 NA KUZIKWA SIKU ILIYOFUATIA YA MACHI 24, 2013 KATIKA MAKABURI YA KISUTU JIJINI DAR ES SALAAM.

MARIJANI ALIZALIWA TAREHE MARCHI 03, 1955 KARIAKOO, JIJINI DAR ES SALAAM. KWA MAPENZI YAKE MUNGU, AKAMCHUKUA AKIWA NA UMRI MDOGO WA MIAKA 40 TU.
ALIKUWA AKITUNGA NA KUIMBA NYIMBO ZILIZOKUWA ZIMEJAA MAUDHUI MEMA KWA JAMII, IKIZINGATIWA KWAMBA TAKRIBAN NYIMBO ZAKE ZOTE ZILIKUWA NI VISA VYA KWELI.
NGULI HUYO ALIKUWA NI MITHIRI YA ‘MTAMBO’ WA KUREKEBISHA TABIA YA MTU YEYOTE ALIYEFANYA MAMBO KINYUME CHA MAADILI PASIPO KUJALI CHEO, URAFIKI, UDUGU HATA UKARIBU.
UBORA WA MASHAIRI KATIKA NYIMBO HIZO, NI KATI YA SABABU ZA KUENDELEA KUPENDWA NA WAPENZI WA MUZIKI HAPA NCHINI HADI KUFIKIA KUITWA ‘JABARI LA MUZIKI’
KILA KUMBI ZA STAREHE UTAKAZOINGIA HAPA NCHINI, NYIMBO ZAKE HAZIKOSI KUSIKIKA ZIKIRINDIMA. HALI KADHALIKA BENDI ZETU ZA MUZIKI WA DANSI ZILIZOSALIA NAZO HAZIWEZI KUMALIZA ONESHO PASIPO KUPIGA ANGALAU WIMBO MMOJA WA NGULI HUYO.  
WASIFU WA MARIJAN RAJABU UNAELEZA KWAMBA MAMA YAKE ALIKUWA MAMA WA NYUMBANI WAKATI BABA YAKE ALIKUWA NA SHUGHULI ZA UCHAPISHAJI.

MAISHA YAKE YA UTOTO YALIKUWA YA KAWAIDA ILA ALIKUWA AKIPENDA SANA UIMBAJI WA TABU LEY, MWIMBAJI TOKA JAMHURI YA KIDEMOKRASIA YA CONGO NA MWIMBAJI TOKA NCHINI GUINEA, SORRY KANDIA. PIA ALIKUWA AKICHEZA MPIRA WA MIGUU.
ALILELEWA KATIKA MISINGI YA DINI YA KIISLAM KWA HIVYO ALIHUDHURIA MAFUNZO YA DINI UTOTONI KAMA INAVYOTAKIWA.

ALIPOKARIBIA  UMRI WA MIAKA 18, NURU YAKE YA KATIKA MUZIKI ILIANZA KUNG’ARA, BAADAYE ALIJIUNGA NA BENDI YA STC JAZZ, IKIWA CHINI YA MPIGA GITAA MAARUFU WAKATI HUO RAPHAEL SABUNI. KABLA YA HAPO,  BENDI HIYO ILIKUWA UNAJULIKANA KAMA THE JETS.
AKIWA KATIKA BENDI HIYO MARIJANI ALIWEZA KUTOKA NJE YA TANZANIA KWA MARA YA KWANZA AMBAPO ALIKWENDA NAIROBI NCHINI KENYA.
KATIKA SAFARI HIYO ALIAMBATANA NA BENDI KWA MADHUMUNI YA KWENDA KUREKODI NYIMBO ZILIZOTOKA KATIKA NEMBO  YA PHILLIPS.
AKIWA NA BENDI HIYO YA STC, UONGOZI WA SHULE YA SEKONDARI YAKE YA TAMBAZA ULILETA MALALAMIKO KWA UONGOZI WA STC ILIYOKUWA IKIMILIKI BENDI HIYO JAMBO AMPALO STC IKALAZIMIKA KUMUENGUA.

MWAKA 1972 MARIJANI ALIHAMIA BENDI YA SAFARI TRIPPERS, ILYOKUWA INAUNDWA NA VIJANA WENZAKE NA HAIKUWA IKIMILIKIWA NA CHOMBO CHA UMMA.

JAMBO PEKEE MARIJANI ALIONEKANA KWAMBA ALIKUWA ‘AMEBANWA’ HUKO STC KATIKA FURSA YA KUNG’ARA KATIKA UIMBAJI, UBORA WAKATI HUO ALIFINGUKA HASWA NA KUWEZA KUINYANYUA SAFARI TRIPPERS KUWA MOJA YA BENDI MAARUFU HAPA NCHINI.

ALIWAKUTA VIJANA WENZAKE AKINA DAVID MUSSA ALIYEKUWA AKIPIGA GITA LA SOLO NA KUIMBA. DAVI HIVI SASA NI MLOKOLE AMEACHANA NA MAMBO YA MUZIKI ANAISHI KARIBU NA KLABU YA TTC CHANG’OMBE.
WENGINE WALIKUWA ALLI RAJABU (MWIMBAJI), CHRISTIAN KAZINDUKI ALIYEKUWA AKILIUNGURUMISHA GITA ZITO LA BESI, JOSEPH BERNARD KWA UPANDE  WA SAXOPHONE NA JEFF AMBAO HADI SASA WANAPIGA KATIKA BENDI YA MLIMANI PARK WALIOJIUNGA NAYO MWAKA 1978.

WALIWEZA KUTOA VIBAO VILIVYOPENDWA MFULULIZO PIA WALIZUNGUKA NCHI NZIMA. VIBAO KAMA ROSA NENDA SHULE, MATILDA, BABA NYERERE MLEZI, MKUKI MOYONI, KUMEKUCHA AMBAO ULIPENDWA NA RADIO TANZANIA DAR ES SALAAM (RTD) NA KUFANYWA KUWA KIAMSHO CHA KIPINDI CHA KUMEKUCHAKILICHOKUWA KIKIRUSHWA KILA CHA ALFAJIRI.

SAFARI  TRIPPERS ILIKUWA KATIKA USHINDANI NA BENDI NYINGINE ZA VIJANA NA HASA AFRO 70, ILIWEZA KUUZA ZAIDI YA NAKALA 10,000 ZA SANTURI NA HIVYO KUWEZESHA BENDI KUNUNUA VYOMBO VYAKE VIZURI AINA YA RANGERS VILIVYOKUWA MAARUFU WAKATI HUO, IKIWA NA MAKAO YAKE MAKUU ENEO LA CHANG’OMBE UHINDINI, TEMEKE JIJINI DAR ES SALAAM.

‘JABALI LA MUZIKI’ MARIJANI ALIHUSUDU KWA KIASI KIKUBWA UIMBAJI WA ALIYEKUWA KIONGOZI WA EMPIRE BAKUBA KABASELE YAMPANYA ‘ PEPE KALE’ HATA BAADHI YA NYIMBO ZAKE ZILIKUWA AKIZIGHANI, ZIKISHABIHIANA NA LADHA YA UIMBAJI WA PEPE KALE.

‘LAKUVUNDA HALINA UBANI’ MSEMO HUU ULIJIONESHA WAZI PALE MAELEWANO MABAYA KATI YA WANAHISA WANNE WA BENDI HIYO, YALIYOPELEKEA KUSAMBARATIKA LICHA YA BENDI HIYO AMBAYO ILIKUWA IKO JUU KIMUZIKI WAKATI HUO MWAKA 1978.

MARIJANI AKIAMBATANA NA WENZAKE KAZINDUKI ‘PACHA’  WAKE KATIKA KUIMBA HATA KUSHABIHIANA MAJINA, ALLY RAJABU, BENARD  NA JEFF WAKAJIUNGA NA BENDI MPYA YA DAR INTERNATIONAL ILIYOKUWA ILIYOONGOZWA NA MPIGAJI GITA LA SOLO ABEL BARTAZAR ALIYEAMBATANA NA GWIJI MWINGINE MUHIDINI GURUMO.
WAKIUNGANA NA WANAMUZIKI WENGINE, MAHIRI WALISHIKAMANA KUUNDA KIKOSI ‘MOTO’ AMBACHO  BAADA YA KUPAKUA ‘VIBAO’ VYAKE VYA KWANZA UKIWEMO WA ‘MARGARET’ WALITIKISA ANGA YA MUZIKI HAPA NCHINI.
KATIKA BENDI HIYO YA DAR INTERNATIONAL WALIKUTA WANAMUZIKI WAZURI NAO WAKAONGEZA  NGUVU NA KUIFANYA BENDI HIYO KUPATA UMAARUFU WA HALI YA JUU KWA VIBAO VYAKE KAMA ZUWENA NA MWANAMEKA, AMBAVYO VILITAMBA KATIKA VIPINDI KADHAA VYA SALAMU VYA RADIO TANZANIA DAR ES SALAAM (RTD) WAKATI HUO.

HALI YA WAKATI ULE, BENDI ILIREKODI VIBAO VYAO  RADIO TANZANIA DAR ES SALAAM (RTD) NA KUAMBULIA SHILINGI 2,500 TU.

YAELEZWA KWAMBA NYIMBO ZAO TISA ZILIUZWA KWA KAMPUNI YA POLYGRAM BILA YA RIDHAA YAO.

KATI YA MWAKA 1979 NA 1986 BENDI ILIPIGA MUZIKI KARIBU KILA WILAYA  HAPA NCHINI KWA MINAJIRI YA KUTOA ELIMU SANJARI NA KUWABURUDISHA WANANCHI WAKIPIGA KATIKA MTINDO WAO WA SUPER BOMBOKA.

MARA NYINGI ILIPOKUWA HAPA DAR ES SALAAM, KAMA ILIVYOKUWA SAFARI TRIPPERS, MAKAO YAKE MAKUU YALIKUWA KATIKA HOTELI YA PRINCESS MNAZI MMOJA, SUPER BOMBOKA LILISAKATWA KILA WIKI, KATIKA UKUMBI WA SUPER FANAKA BUGURUNI.

‘MBIO ZA  SAKAFUNI HUISHI  UKINGONI’ UCHAKAVU WA VYOMBO HATIMAE MWAKA HUO 1986, UKAMALIZA MBIO NDEFU ZA BENDI HII.

MARIJANI RAJABU ‘JABARI LA MUZIKI’ ALIKUWA MMOJA KATI YA WANAMUZIKI 57 WALIOUNDA KUNDI LA WASANII LIKIJULIKANA KAMA TANZANIA ALL STARS, MWAKA 1987.

KUNDI HILO LILITIA FORA MKWA WIMBO WAKE WA ‘FAGIO LA CHUMA’  WIMBO HUO ULIKUWA NI KUITIKIA KAULIMBIU YA RAIS WA AWAMU YA PILI ALI HASSAN MWINYI, JUU YA UWAJIBIKAJI.

KUNDI HILO LILIREKODI VIBAO VINGINE VINNE AMBAVYO SI RAHISI KWA BENDI ZILIZOPO SASA KUFIKIA UBORA WAKE KIMUZIKI.

KUNA WAKATI DAR INTERNATIONAL ILISIMAMA KIMUZIKI, MARIJANI ALISHIRIKI KUPIGA MUZIKI KATIKA BENDI YA JESHI LA WANANCHI TANZANIA (JWTZ) YA MWENGE JAZZ AMBAKO ALIPIGA MUZIKI  KWA MUDA MFUPI.

MARIJANI ALIPIGA HODI KATIKA JIJI LA ARUSHA NA KUJIUNGA NA BENDI YA KURUGENZI JAZZ AMBAKO HUKO ALIDUMU MWAKA MMOJA PEKEE NA KUREJEA DAR ES SALAAM.

MFANYABIAHARA MMOJA WA JIJINI DAR ES SAAM ALIYEJULIKANA KWA JINA ROGER MALILA,ALIMCHUKUWA MARIJANI KWA AJILI YA KUANZISHA BENDI YA ORCHESTRA BENE BENE. BENDI HIYO WAKATI HUO ILITAMBA NA MTINDO WAKE WA ‘MAHEPE’ MWANZONI MWA MIAKA YA 1990.

MARIJANI KWA MARA NYINGINE TENA BAHATI HAIUKUWA UPANDE WAKE, KWANI BENDI HIYO HAIKUDUMU KWA KIPINDI KIREFU KUFUATIA UKOSEFU WA VYOMBO VYA MUZIKI. HATIMAYE MAMBO YAKAENDA KOMBO TOFAUTI NA WALIVYOTARAJIA.

BAADA KUHANGAIKA KWA MUDA MREFU  HUKU NA KULE MARIJANI ‘JABARI LA MUZIKI’ ALIAMUA KUTHUBUTU KWA KUANZISHA KUNDI LAKE LA MUZIKI LIKIITWA AFRICULTURE.
LAKINI NAYO HAIKUDUMU NAYO IKAFA ‘KIFO CHA MENDE.’

MAISHA YA MWANADAMU NI KITENDAWILI KILICHOJAA MAJARIBU MENGI.
INAELEZWA KWAMBA KUFIKIA MWAKA 1992, HALI YA MAISHA YA MARIJANI ILIKUWA NGUMU KUPITA KIASI. ALIFIKIA KUENDESHA MAISHA YAKE KWA KUUZA KANDA ZA NYIMBO ZAKE. ALIJENGA KIBANDA NJE YA NYUMBA YAKE, MAENEO YA KARIAKOO, JIJINI DAR ES SALAAM.

PAMOJA NA NYIMBO NYINGI, ZA KUIMBIA CHAMA TAWALA NA SERIKALI, NA HATA TUNGO YAKE MWANAMEKA KUTUMIWA KATIKA MTIHANI WA KIDATO CHA NNE, MARIJANI RAJABU HADI SEPTEMBA 09, 2012  NDIPO RAIS DK. JAKAYA KIKWETE ALIPOMTUNUKIA TUZO YA HESHIMA YA MUUNGANO KATIKA MAADHIMISHO YA MIAKA 51 YA UHURU  IKULU JIJINI DAR ES SALAAM.

WASANII WENGINE WALIOTUNUKIWA SIKU HIYO NI PAMOJA NA KIONGOZI WA ZAMANI WA MSONDO NGOMA, MUHIDINI GURUMO, MWIMBAJI WA MKONGWE  WA TAARABU, FATUMA BINT BARAKA, MSANII WA MAIGIZO YA FILAMU, FUNDI SAID ‘MZEE KIPARA’ NA MWANARIADHA MKONGWE JOHN STEVEN AKWARI.

HAPANA SHAKA UTAKUWA UNAZIKUMBUKA NYIMBO ZA NGULI HUYU ALIZOTUNGA NA ZINGINE KUSHIRIKI KIKAMILIFU KUIMBA KAMA VILE MASUDI, HABARI YAKO, SAUTI YAKO NYORORO, BABA ANNA, KITINDA MIMBA, SALAMA NAKUITA, NAMSAKA MBAYA WANGU, ZUWENA NA NDOA YA MATESO.

MARIJANI RAJABU HAKUISHIA HAPO KWANI ALITOKA NA NYIMBO ZANGINE ZA TABU NI HALI YA DUNIA, NDOA YA MATESO, NAMSAKA MBAYA WANGU, MAMA WATOTO, TAMAA MBELE NA BABA WATOTO AMBAZO ZILIGUSA HISIA ZA  WAPENZI WA MUZIKI NA WALE WAKAWAIDA WALIOKUWA WAKISIKILIZA REDIO.
NYIMBO WA ‘UKE WENZA UNA MAMBO’, ULIOFYATUA, NDOA NYINGI ZA MITARA ZILIJIREKEBISHA KITABIA.
WIMBO WA GEORGINA ULIKUWA WIMBO ULIOTIA FORA MIONGIONI MWA NYIMBO BORA HAPA NCHINI.

MTUNZI WA WIMBO HUO WA GEORGINA ALIKUWA WANAMUZIKI MKUNG’UTAJI GITA LA RHYTHM MAHIRI NCHINI JUMANNE UVURUGE, UKAIMBWA KWA UMAHIRI MKUBWA KWA SAUTI YENYE HISIA KALI NA MARIJANI RAJABU.

MARIJANI ALITHUBUTU KUKEMEA TABIA MBOVU YA NDUGU YAKE WA KARIBU KUPITIA WIMBO WA ‘CHAKUBANGA’.  WIMBO HUO ULIKUWA NI KISA CHA KWELI AMBACHO NDUGU YAKE HUYO BAADA YA KUTOKA ULAYA, AKAJIITA JOHN SMITH BADALA YA JINA LAKE HALISI LA CHAKUBANGA.

KUPATA LADHA HALISI YA WIMBO HUO, SEHEMU FUPI YA GHANI ZAKE KATIKA KIBAO CHA CHAKUBANGA NI KAMA IFUATAVYO:

“LEO KIJANA NINASEMA EEH! HAYO MAMBO YAKO UNAYOFANYA EEH, MWISHO WAKE BWANA, MAMBO YATAKUWA MABAYA, WALA USIDANGAYIKE NA CHEO ULICHOPATA, KUDHARAU WAZAZI KUHADAIKA NA DUNIA, MWANA VIBAYA EEH, VIBAYA MWANA VIBAYAA.

“FIKIRI KWANZA ULIKOTOKAA, USIJIFANYE HUNA BABA WALA MAMA WALIO KULEA, KWA TAABU NYINGI NA MASHAKA , WAKAKUSOMESHA UKAHITIMU MAFUNZO, MBONA UNAWANYANYASA NA MATUSI KUWATUKANAAA, MWANA VIBAYAA, VIBAYA MWANA VIBAYAA. MAMBO YA AJABU ULIYOFANYA EEH, ULIPOCHAGULIWA KWENDA NG’AMBOO ULIPORUDU BWANA, NA JINA UMEBADILISHA, JINA LAKO CHAKUBANGA, UNAJIITA JOHN SMITH, NA MWENDO UMEBADILI BEGA MOJA UMELISHUSHA…”
NYIMBO ZA  NGULI HUYU ZITAENDELEA KUSIKIKA VIZAZI NA VIZAZI KWAKUWA ZIMEBEBA UJUMBE MZITO KWA JAMII YEYOTE ILE.

JE, TUNAMUENZIJE MARIJANI RAJABU? USHAURI  WANGU KWA VIJANA WA MUZIKI WA KIZAZI KIPYA KUFUATA NA KUYAENDELEZA YOTE MAZURI YA WATANGULIZI WAO KAMA AKINA MARIJANI, GURUMO, MBARAKA MWINSHEHE NA WENGINE WENGI.

MUNGU AIWEKE ROHO YAKE PAHALA PEMA PEPONI, AMINA.

MWISHO.