Monday, June 20, 2016

ALLI JAMWAKA ALIYEIKANYAGA ARDHI YA MAREKANI WA KUPIGA TUMBA



ALLI JAMWAKA ALIYEIKANYAGA ARDHI YA MAREKANI WA KUPIGA TUMBA

Miaka ya 1980 hadi 1990 walikuwepo wadunda tumba wengi waliosifika katika bendi za muziki hapa nchini.
Katika bendi ya Maquis du Zaire alikuwepo Pulukulu Wabandoki Motto, aliyekuwa kivutio kikubwa kwa wapenzi na mashabiki wa bendi hiyo. Halikadhalika bendi ya MK Group alikuwa mpiga tumba maarufu Sidy Morris ambaye wakati wa uhai wake alikuwa akionesha madoido ya wakati akilizidunda tumba kwenye ukumbi uliokuwepo katika hoteli ya New Afrika jijini Dar es Salaam hadi wakampachika jina bandia la ‘Tanzania One’,
Miaka ya 2000 alijitokeza mpiga tumba aliyekuwa katika bendi ya African Stars, MCD ambaye aliweza kuwachezesha wanenguaji akipiga tumba huku akipuliza filimbi.
Katika makala haya yanamzungumzia mpiga tumba Ally Omary Jamwaka, aliyejizoela sifa nyingi kwa uhodari wake wa kupiga tumba.
Wasifu wa Jamwaka unaeleza kuwa  alizaliwa katika kijiji cha Malui Machi 01, 1953. Alijiunga na shule ya msingi ya kijijini kwake kuanzia mwaka 1960 hadi alipomaliza elimu ya darasa la saba.
Mwaka 1969 akaingia katika jiji la Dar es Salaam akaanza kutafuta maisha. Alli Jamwaka alikuwa na ndoto za kuwa msanii. Hiyo yawezeka alivutiwa na jinsi kaka yake Shaaban Omary Jamwaka alikuwa mpiga drums ambaye aliyetangulia kufika katika jiji hilo.
Kaka yake huyo ndiye aliyechangia kwa kiasi kikubwa kumtia hamasa ya kuwa msanii.
Jamwaka amekuwa kwenye talanta hiyo tangia miaka ya 1970 mara baada ya kujiunga na kikundi cha sanaa kilichokuwa na maskani maeneo ya Buguruni, jijini Dar es Salaam, kikiwa chini ya Mzee Mindu.
Akiwa na kikundi hicho ndipo alipokutana na rafiki yake aliyeitwa Adam Bakari, huyu baadae sana alikuja kupewa jina la ‘Sauti ya Zege’.
Kwa pamoja wakajadiliana jinsi ya kujikwamua kimaisha wakaamua kutengeneza kundi lao waliloliita The Hippies.
Kundi hilo lilikuwa ni la muziki wa vijana lililokuwa na kazi ya kwenda kwenye kwenye kumbi za madansi kunakopiga bendi kubwa, na kuomba 'ujiko' ili waoneshe makali yao.
Mtindo ulikuwa wa kawaida kwa vijana waliokuwa wakichipukia katika muziki, ulikuwa umeenea nchi nzima wakati huo. Bendi ndogo zilikuwa zikifuatilia zinakopiga bendi kubwa nao kuomba nafasi kidogo.
Walivyokuwa wakiruhusiwa kupiga nyimbo kadhaa walikuwa wakitumia vyombo  vya bendi kubwa. Mtindo huo uliwapa uzoefu vijana hao. Walionekana kuwani wazuri walipatiwa hata kupata ajira papo hapo.
Bendi ya The Hippies ilikuwa imeweka makao makuu yake mtaa wa Somali maeneo ya Kariakoo, jijini Dar es Salaam. Walikuwa wakipiga muziki wa kukopi bendi za ndani na nje zilizotamba wakati huo, hasa zile za Ulaya na Marekani. Jamwaka wakati huo alikuwa tayari akipiga tumba na drums.
Miaka ya 1970 Mashirika ya Umma yalianzisha vikudi mbalimbali vya sanaa zikiwemo bendi. Alli Jamwaka  alijiunga mwaka 1971 katika bendi ya Biashara Jazz.
Biashara Jazz wakati huo ilikuwa bado mpya kabisa baada ya kubadili jina kutoka STC Jazz. Bendi hiyo ilikuwa chini ya mmiliki ya Board of Internal Trade (BIT) ambayo chini yake kulikuwa na mashirika ya umma kama RTC, DABCO, HOSCO, GEFCO na kadhalika.
Katika bendi hiyo aliwakuta akina wanamuziki wengine akina Raphael Sabuni, Belino, Muddy, na kaka yake Shaaban Omary Jamwaka ambaye alikuwa mpiga drum wa bendi hiyo wakati huo.
Ally Jamwaka alipiga muziki katika bendi  hiyo chini ya uongozi wa Juma Ubao ‘King Makusa’ hadi mwaka 1977 alipoamua kujiunga katika bendi ya Tanzania Stars.
Bendi hiyo ilikuwa na makao yake katika ukumbi maarufu miaka hiyo iliyoitwa Margot ambayo ilikuwa katikati ya Jiji pembeni mwa barabara ya Samora jijini humo.
Ukumbi huo ulikuwa maarufu mno kwakuwa muziki ulikuwa ukipigwa kila siku mpaka usiku wa manane.
Wateja wakubwa Margot walikuwa ni  mabaharia walikuwa wakisha tia nanga meli zao katika bandari ya Dar es Salaam, usiku walikuwa wakijazana Margot ambako kulikuwa ni mahala penye starehe za kila aina.
Kufika kwake bendi hiyo alipishana na wanamuziki maarufu ambao wote ni marehemu, Haruna Lwali mpiga tumba na Joseph Bartholomew Mulenga ‘King Spoiler’ aliyekuwa akipiga gitaa, waliohamia bendi ya Orchestra Santa Fe, iliyokuwa ikipiga muziki katika ukumbi jirani wa Gateways.
Baadhi ya wanamuziki waliokuweko katika bendi ya Tanzania Stars wakati huo walikuwa Joseph Emmanuel aliyekuwa akiimba na kupiga gitaa, Hussein Sadiki na Yahaya Bushiri. Bendi hiyo ilikuwa inapiga muziki ya kukopi kutoka nchi mbalimbali duniani, kuwaburudisha wateja wao  hasusani mabaharia kutoka kila kona ya dunia.
Wakati huo ilikuwa ukiingia katika ukumbi wa Margot ungeweza kusikia nyimbo za Kichina, Kihindi, Kigiriki na ngine toka mataifa mbalimbali duniani.

Baada ya ukumbi huo kuchukuliwa na Chama Cha Ushirika, bendi pia ikachukuliwa, na ndipo ilipozaliwa ile bendi maarufu ya Washirika Tanzania Stars. ‘Wantunjatanjata’
Alli Jamwaka alichukuliwa akajiunga  kupiga muziki katika bendi hiyo mpya ya Tanzania Stars mpaka mwaka 1979.
Uongozi wa bendi ya Orchestra Mlimani Park ulimfukuza kazi mpiga tumba wake aliyekuwa akiitwa Haruna Lwali, na hapo Abel Balthazar aliyekuwa mmoja kati ya viongozi wa bendi hiyo, alimfuata Jamwaka ili ajiunga katika bendi ya Orchestra Mlimani Park Orchestra.

Mlimani Park  ilikuwa chini ya Chama cha Usafirishaji na hasa wa Taxi (TTTS).
Bendi ya Orchestra Mlimani Park Bendi ilipewa huduma nzuri sana hadi  kufikia kuwa moja ya bendi kubwa nchini. Nyimbo zake za wakati ule bado zinaheshimika katika nyanja za muziki hata leo.
Ukumbi wa Msasani Beach Club ulikuwa mmoja wa mali za TTTS, na bendi ya Mlimani Park ndio iliyojenga ukumbi huo kwa kutumia mapato ya kila Jumatano kuelekezwa kwenye ujenzi wa ukumbi huo. Baada ya ukumbi huo kukamilika wanamuziki wakiwa na imani ambayo baadae ilikuja kuonekana potofu, waliamua kutumia fedha yao ya kila Jumatano kuanza kujenga ukumbi wa bendi yao uliokuwa Mpakani, maeneo ya Mwenge jijini Dar es Salaam.
Lakini taharuki iliyojiri wakati huo, ujenzi ulifika mahala ukadorora na kufa kabisa.
Mwaka 1982 mali za TTTS kama vile bendi na ukumbi wa Mpakani ukahamishiwa Shirika la Maendelo la Jiji la Dar es Salaam (DDC).
Awali kulikuweko na wazo kuwa bendi hiyo ihamishwe kuwa chini ya Shirika la Ndege Tanzania (ATC) maana wakati huo Shirika hilo lilikuwa na klub yao moja nzuri.
 Lakini ikaonekana DDC walikuwa na kumbi nyingi zikiwemo za DDC Kariakoo, DDC Magomeni Kondoa na  DDC Keko. Ilielezwa kwamba bendi Mlimani Park Orchestra ingefanya kazi kwa ufanisi zaidi huko.
Kwa mantiki hiyo bendi pamoja na  wanamuziki wakauzwa kwa Shirika la Maendeleo la Dar es Salaam (DDC).

Walipiga muziki katika bendi hiyo hadi mwaka 1985, ambapo awamu ya kwanza ya kundi kubwa la wanamuziki lilipoondoka DDC Mlimani Park Orchestra na kujiunga na kundi lililoanzishwa la International Safari Sound.
Bendi hiyo ikapewa majina ya Orchestra Safari Sound (OSS),
iliyokuwa na mtindo wa ‘Ndekule’.
Baadhi ya wanamuziki walikuweko ni pamoja na Abel Barthazar, Muhidin Maalim Gurumo, Ally Makunguru, Mustafa Jonh Ngosha, Kassim Rashid ‘Kizunga’ pamoja na mwimbaji mahiri Skassy Kasambula.
Katika awamu ya pili ya wimbi la wanamuziki wa Orchestra Mlimani Park walichomoka kwenda Orchestra Safari Sound, Ally Jamwaka pia alikuweko.
Wakati waimbaji mashuhuri akina Fresh Jumbe, Cosmas Chidumule, Hamis Juma ‘Maalimu Kinyasi’ na mcharangaji drums Chipembele Said ‘Bobchipe Chipembele’, wakasindikizana na Michael Bilali ambaye alirejeshwa Orchestra Mlimani Park kwa nguvu ya wapenzi na mashabiji wa bendi hiyo  waliochanga fedha na kulipa fedha alizokuwa kachukua toka uongozi wa Orchestra Safari Sound.
Alli Jamwaka amewahi kufanya ziara nyingi ndani nan je ya nchi. Ziara ambayo iliweka historia katika maisha yake ni ile alipopata fulsa miaka michache ya nyuma kwenda Marekani kupiga muziki akifuatana na wanamuziki wengine akiwemo Hassan Rehani Bichuka.
Mwisho.

KASSIM MPODA ‘De la Chance’ ATIMIZA MIAKA 14 KABURINI



KASSIM MPODA ‘De la Chance’ ATIMIZA MIAKA 14 KABURINI

Wapenzi na mashabiki wa  muziki wa dansi hususani katika jiji la Dar es Salaam, jina la Kassim Mponda ‘De la Chance’  lilikuwa maarufu mnamo miaka ya 1980 na 1990, akipiga katika bendi za Juwata na Mlimani Park.
Mwanamuziki huyo alikuwa mpiga gitaa mashuhuri hapa nchini, Juni mwaka huu 2016, imetimia miaka 14 tangu alipofariki mwezi Juni 2002 akiwa katika jiji la Dar es Salaam.
Wakati wa uhai wake alijizolea sifa lukuki kwa kulicharaza gitaa la besi na solo kwa nyakati tofauti.
Alionesha makali yake hususani alipokuwa katika bendi ya Juwata. Gitaa lake hilo lilisikika kwenye wimbo wa Sogea Karibu.
Katika wimbo huo Waziri Alli alibofya kinanda kwa umahiri mkubwa sana.
Wasifu wa Mponda unaleleza kuwa alikuwa wa kabila Kindengereko aliyezaliwa mwaka 1945, barabara ya Mwanza mjini Tabora. Mwaka huo una historia kubwa duniani kote kwani ulikuwa mwaka ambao Vita vikuu vya pili vya dunia vilipomalizika.
Majina yake halisi alikuwa akiitwa Kassim Mponda Mbwana. Baba yake mzazi Mbwana Mponda aliyekuwa na asili ya Kabila la Kindegereko toka mkoa wa Pwani.  Mzee Mponda alifika Tabora na kuwa mfanyabiashara ndogondogo.
Kassim Mponda alipata elimu ya msingi katika shule ya Town, iliyopo mjini humo, baadaye alijiendeleza mwenyewe kujifunza lugha ya Kiingereza.
Alifunzwa kupiga gitaa la besi akiwa nyumbani kwa Hassani Athumani, aliyekuwa mwanamuziki katika bendi za Tabora Jazz, Kiko Kidds, Nyanyembe Jazz na Milambo ‘ Wana Sona sona’ kwa nyakati tofauti.
Hassan Athumani ambaye hivi sasa ni mjasiliamali akitengeneza Samani za ndani nyumbani kwake Barabara ya Mwanza mjini humo, aliunda kikundi kidogo cha vijana waliokuwa wanapenda kufundishwa muziki.
Kikundi hicho kilikuwa kikipiga muziki ‘mkavu’, vyombo vya muziki vilivyokuwa vikitumika ni magitaa makavu na ngoma.
Baadhi ya vijana walioshiriki kwenye kikundi hicho ni pamoja na yeye Hassani Athumani, aliyekuwa akilicharaza gitaa la solo, Kassim Mponda akiliungurumisha gita zito la besi na ngoma zilidundwa na Mavumbi Alli. Kwa upande wa waimbaji walikuwapo Hassani Athumani, Bozeni na Moshi Alli. 
Baadaye Mponda alikwenda kujiunga na bendi ya Kiko Kidds, iliyokuwa ikiongozwa na Salim Zahoro, mjini Tabora. Wakati huo huo mwalimu wake Hassani Athumani alikwenda kujiunga katika bendi ya Tabora Jazz.
Baada ya miezi takribani mitatu, Kassim Mponda aliicha bendi hiyo na kuchepukia katika bendi ya Tabora Jazz, akamfuata mwalimu wake Hassani Athumani.
Akiwa katika bendi hiyo, Mponda alionesha makali yake vilivyo kwa kuliungurumisha gitaa la besi wakati huo.
Kati ya mwaka 1968 na 1966, aliondoka katika bendi ya Tabora Jazz, akaenda katika jiji la Dar es Salaam ambako huko alijiunga katika bendi ya Western Jazz hadi mwaka 1967, aliporejea tena Tabora.
Alipofika mjini humo alimkuta Hassan Athumani akiwa mbioni kuanzisha bendi mpya ya Nyanyembe Jazz. Aliungana naye kuwa mmoja wa waanzilishi wa bendi hiyo.
Akiwa na Nyanyembe Jazz, Mponda ndipo alianza kupiga gitaa la solo hadi Juni 1967, alipoondoka kwenda Dodoma kujiunga katika bendi ya Central.
Alikuwa na sifa kubwa ya utafutaji maendeleo latika muziki hivyo baada ya miezi miwili alikwenda Dar es Salaam kujiunga katika bendi ya Polisi Jazz. ‘Wana Vangavanga’.
Akiwa katika bendi ya Polisi Jazz alikokutana na aliyekuwa kiongozi wa bendi hiyo Kassim Mapili. Licha ya kuwa kiongzi Mapili pia alikuwa ni mtunzi, mwimbaji na uwezo mkubwa wa kupiga gitaa.
Hukaa sana katika bendi hiyo baada ya kipindi kifupi Mponda aliondoka akaenda kujiunga katika bendi ya Vijana Jazz iliyokuwa ikiongozwa na Hemed Maneti wakati huo.
Hata huko Viajana Jazz nako hakutumikia kwa kipindi kirefu kwani alitimka kwenda kujiunga katika bendi ya Safari Trippers, ambako katika wimbo wa Salama alikung’uta gitaa ‘kinoma’ likisindikiza sauti nyororo ya Marijani Rajabu wakati huo.
Baadaye akawa mmoja kati ya wanamuziki waloihama Safari Trippers, wakaenda kuanzisha bendi ya Dar International.
Bendi ya Juwata ‘Wana Msondo ngoma’ ilimyakuwa Kassim Mponda kuongeza nguvu katika bendi yao.
Wakati huo bendi ya Juwata ilikuwa ikipiga kwenye ukumbi za Kigongo Bar, maeneo ya Buguruni na Argentina maeneo ya Manzese jijini Dar es Salaam.
Mnamo miaka ya 1980 Kassim Mponda alijiunga katika bendi ya Orchestra Mlimani Park akitokea Msondo ngoma na baadaye alichukuliwa kwenda kupiga muziki katika bendi ya African Sound Orchestra (Afriso Ngoma).
Bendi hiyo ilikuwa ikiongozwa na mtunzi na mwimbaji mahiri toka Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo, Lovy Longomba.
Longamba aliwahi kukiri umahiri wa Kassim Mponda tangu akiwa katika jiji la Nairobi miaka ya 1980, alimuelezea kuwa ni mmoja wa wapiga solo wa Kitanzania anaowaheshimu sana pamoja na kwamba alikuwa hajawahi kukutana nae.
Sifa hizo ndizo ilielezwa kuwa yawezekana ndio zilimfanya Lovi amchukue kujiunga katika bendi ya Afriso.
Wakati huo Lovi Longomba alikuwa ni ,wanamuziki katika bendi ya Super Mazembe, iliyokuwa na makazi yake katika  jiji la Nairobi nchini Kenya.

Kwa upande wake Mponda hakuwa akitarajia sifa kubwa toka mwimbaji na mtunzi katika bendi ya Super Mazembe.
Akisimulia wasifu wa Mponda, Hassani Athuani alisema kuwa kuondoka kwa Mponda katika bendi ya Juwata, kulipelekea bendi hiyo kumchukua mwanamuziki chipukizi Abdu Ridhiwani Pangamawe kujaza nafasi yake.
Pangamawe aliingia katika bendi hiyo akiwa na vipaji vingi kikiwemo cha kulicharaza gitaa la solo na kubofya kinanda. Ikumbukwe kwamba hata wakati mbofya kinanda wa bendi hiyo Waziri Alli ‘Kissinger’ alipoondoka kwenda katika bendi ya Kilimanjaro ‘Wana Njenje’, Ridhiwani aliziba nafasi yake pasipo shaka.
Mponda aliyepachikwa jina la bandia la ‘De la Chance’, likiwa na maana ya ‘mtu mwenye bahati’.
Ndiye aliyepiga gitaa solo katika nyimbo nyingi ukiwemo wa wa Kiu ya Jibu, Ashibai, Sogea Karibu na vingine vingi akiwa na bendi ya Mlimani Park Orchestra.
Nyota ya Mponda ilianza kufifia baada ya kuondoka katika bendi ya Juwata hata alipokwenda kujiunga na bendi za  Mlimani Park, Bima Lee na hatimaye Afriso Ngoma.
Aidha gitaa lake linasikika vizuri katika wimbo wa ‘Dawa ya Pendo ni Pendo’ uliofyatuliwa na bendi ya DDC Mlimani Park Orchestra.
Mponda alikuwa ni miongoni mwa wanamuziki waliochukuliwa na Shirika la Bima la Taifa kwenda kuongeza nguvu katika bendi ya Shirika hilo ya Bima Lee Orchestra. Bima Lee ilikuwa ikitumia mtindo wa ‘Magneto tingisha’
Baadhi ya wanamuziki alioungana nao wakati huo walikuwa ni Jerry Nashon ‘Dudumizi’, Shabani Dede, Joseph Bartholomew Mulenga ‘King Spoiler’, Maximilian Bushoke na wengine.
Katika wimbo wa ‘Busu pande tatu’ ulioghaniwa kwa umahiri mkubwa na Jerry Nashon, Mponda aliyelikung’uta gitaa la rhythm linalosikika, likitanguliwa na solo la Joseph Mulenga.
Aidha kwa kipindi kifupi aliwahi kupiga muziki katika bendi ya Shikamoo Jazz inayoongozwa na Salim Zahoro katika jiji la Dar es Salaam.
Sifa nyingine za Mponda aliyokuwa nayo ambayo wanamuziki wengine wameikosa ni utanashati wake. Alikuwa akionekana maridadi muda na popote utakapokutana naye.
‘De la Chance’ alikuwa akipendelea kuvaa kofia ya aina ya ‘Kapelo’, wakati akishika ‘mpini’ alikuwa akifuata miserebuko ya mashabaki utadhani anawaona rohoni.
Faida ya kuwa na mtoto mwenye hekima aliionja pale mwanae mmoja alipoamua kumnunulia vyombo va muziki vilivyomuwezesha kuanzisha bendi yake ya Afriswezi.
Bendi hiyo iliwahi kufanya ziara mkoani Lindi ambako mara walipowasili mjini humo, Mponda alipatwa na matatizo ya kuziba mkojo yaliyopelekea kulazwa katika hospitali ya wilaya ya Lindi wakati huo.
Juhudi za kumtibu ziliedelea hata kupelekwa Kisiwani Mafia, mkoani Pwani kwa matibabu zaidi. Hata hivyo ilishindikana akarejeshwa jijini Dar es Salaam, ambako aliendelea kupatiwa tiba japo hazikumsaidia hatimaye mwaka 2002, akafariki.

Mungu ailaze roho yake pahala pema peponi, Amina.

Mwandishi wa makala haya anapatikana kwa namba 0784331200 na 0767331200.