Wednesday, December 24, 2014

MIAKA 50 YA MSONDO NGOMA.

MIAKA 50 YA MSONDO NGOMA.



Bendi ya Msondo ngoma Oktoba 10, 2014 imeadhimisha miaka 50 toka ianzishwe mwaka 1964.
Mapema mwaka 1963 Muhidini Gurumo aliitwa kujiunga na NUTA Jazz akitokea katika bendi ya Rufiji Jazz, na kuwa mmoja wa waasisi wa bendi hiyo.
Katika mahojiano maalumu na Mzee Gurumo aliwahi kusema kuwa mpiga solo Ahmed Omar kuwa ndiye aliyechagualiwa kuwa kiongozi wa NUTA Jazz wakati huo.

Walipoanza walikuwa chini ya udhamini wa Chama cha Wafanyakazi Tanzania (National Union of Tanzania) kwa kifupi NUTA. Hivyo bendi ikapewa jina la NUTA Jazz.
Wakati huo iliongozwa na mpuliza Tarumbeta, Joseph Lusungu akisaidiana na Mnenge Ramadhani aliyekuwa akipuliza Saxophoni ‘mdomo wa Bata’.
Miaka michache ya nyuma Chama cha Wafanyakazi kilijitoa kuidhamini na kuwaacha wanamuziki kujitegemea na sasa inaitwa Msondo Ngoma Band, ikiwa ni kuenzi mtindo ilioipa  umaarufu.
Alipojiunga  na bendi hiyo Mzee Gurumo alionesha cheche zake za kwanza kwa kurekodi nyimbo akiwa na NUTA Jazz.  Nyimbo hio zilikuwa za ‘Baba Nyerere’  uliokuwa ukimsifia Mwalimu Nyerere kuleta Uhuru wa Tanganyika. Nyingine ni  ‘Kilimo ni Kazi yetu’ , ‘Mwengele’ na nyingine nyingi.

Nyimbo nyingine zilizotamba zilikuwa za Mpenzi Sofia, Tumeishi toka zamani, na Walinicheka. Zingine zilikuwa Aziza, Tukiwa na Monica shuleni, Sakina , Maneno ya Nyerere, Mipacha Ngui na nyingine nyingi.

Bendi hiyo baadaye ikabadili jina na kuwa ‘JUWATA Jazz’ baada ya jina la Chama cha NUTA kubadilishwa kuwa Jumuiya ya Wafanyakazi Tanzania JUWATA. Hivyo bendi ikawa JUWATA Jazz.

Wakati huo huo mpiga Solo Saidi Mabera alichaguliwa kuwa kiongozi wa bendi hi. Bendi hiyo ikatunga nyimbo nyingi kati ya miaka ya 1980 wakitumia mtindo wa Msondo Ngoma ‘Magoma Kita Kita’
Baadhi ya wanamuziki waliounda JUWATA ni pamoja waimbaji  Muhidin Gurumo aliyeingia katika bendi hiyo iakitokea katika bendi ya Rufiji Jazz, Hassani Rehani Bichuka, na mpiga Kinanda  Waziri Alli ambaye hivi sasa ni mmoja kati ya viongozi wa bendi ya The Kilimanjaro Band. (Wana Njenje).
Ushindani kati ya bendi za muziki wa dansi ulipoongezeka, wanamuziki wawili Muhidini Gurumo na  Hassani Rehani Bichuka waliiacha bendi hiyo na kwenda kujiunga na bendi ya DDC Mlimani Park Orchestra.
Mzee Gurumo alirejea tena JUWATA mwaka 1991 akateuliwa kuwa kiongozi wa bendi hiyo. Nyimbo walizotoka nazo zilikuwa za Nidhamu ya kazi, Ete, Queen Kasse, Mariamu ninakujibu, Usia wa baba, Msafiri kafiri, Tupa tupa, Ndugu Kassimu na nyingine lukuki.

Baadaye bendi hiyo ilibadilishwa tena jina na kuwa OTTU Jazz kufuatia kubadilika kwa jina la Chama cha Wafanyakazi JUWATA kuwa OTTU.
OTTU Jazz au kwa jina lingine wakajiita ‘Baba ya Muziki’ ilitikisa jiji la Dar es Salaam na sehemu nyingine hapa nchini na kuwa tishio kwa bendi zingine.
Wakiwa Dar es Salaam walikuwa wakipiga muziki kwenye ukumbi wa Amana uliopo Ilala. Ilisheheni wanamuziki kabambe akina  TX Moshi William, Nicko Zengekala, Selemani Mbwembwe, Joseph Maina, Mustafa John Ngosha, Suleimani Mwanyiro, Tino Maselenge ‘Arawa’,  Athuman Momba, Abdull Ridhiwan na Roman Mng’ande ‘Romario’
Wengine ni Salehe Bangwe, na bila kuwasahau Huruka Uvuruge na mzee mzima Said Mabera mpiga solo mahiri ambaye tangia ajiunge katika  bendi hiyo hajathubutu kuiondoka.
Shabani Dede alirejea tena katika bendi hiyo akitokea bendi ya Mlimani Park Orchestra (Wana Sikinde).
Kufuatia Hospitali ya Ilala kupanuka, OTTU Jazz walitakiwa kuondoka kwa kile kilichodaiwa ni kuwabughudhi wagonjwa kwa makelele ya vyombo vya muziki wao.
Walilazimika kuhamia ukumbi wa AfriCenter uliopo barabara ya Kigogo, ambako nako hawakudumu kipindi kirefu. Hivi sasa wanapiga muziki wao katika ukumbi wa Max Bar uliopo Ilala Bungoni.
Baadhi ya nyimbo ‘zilizogongwa’ na OTTU Jazz zilikuwa za Kicheko, Mawifi mnanionea, Ndoa Ndoana, Nimezama katika dimbwi, Mti mkavu na Mizimu. Zingine ni Wabakaji, Tabu, Pricila, Penzi la mlemavu, Piga ua talaka utatoa, Tuma, Wapambe, Asha mwana Sefu, Ajali, Mtanikumbuka, Barua ya kusikitisha, Mwana mkiwa,  Kalunde, Kaza moyo, Jesca, Kwenye penzi, Binti maringo, Dalili na nyingine nyingi.
Chama cha Wafanyakazi Tanzania baadaye kijiondoa katika ufadhili wa bendi hiyo, kikawaachia vyombo wajitegemee. Walijikusanya kutengeneza mikakati na kuamua kuipa jina jipya la Msondo Ngoma Band.
Bendi ya Msondo Ngoma imesheheni wanamuziki wengi wakiwemo wa zamani na wapya, wanaofikisha idadi yao kuwa 18 na fundi mitambo mmoja.
Safu nzima ya wanamuziki hao ni Kiongozi wao ni Saidi Mabera ambaye  pia ni mpigaji wa gita la Solo. Waimbaji akaina Juma Katundu, Shabani Dede, Twaha Mohamed, Hassan Moshi William ‘TX Junior’ na Hussein Kalembo.
Wakung’utaji magita ya solo na rhythm ni Ridhiwani Pangamawe na Huruka Uvuruge. Ramadhani Zahoro Bangwe na Mustafa Hamis ‘Pishuu’ hupiga gita la Rhythm. Kwa upande wa gita zito la besi wapo Ally Lindunga na Saad Ally ‘Sure Boy’. Drums huchanganywa na Saad Ally ‘Mashine’ na Arnold Kang’ombe. Tarumbeta hupulizwa na kijana machachari Roamn Mng’ande na Hamis Mnyupe.
Dorice George hupiga Tumba, Drums pia ni Mwimbaji wakati Amiri Said Dongo naye ni mpigaji wa Tumba.

Dorice George ni mwanamuziki mpya wa kike mwenye vipaji vingi. Ni tunda la Chuo cha Sanaa Bagamoyo, bado yupo kwenye majaribio.
Fundi wao wa mitambo anajulikana kwa jina la Mifupa.
Katika orodha ya wanamuziki wa bendi hiyo imewaacha akina Eddo Sanga ambaye ni mwimbaji na Shabani Lendi mpulizaji wa  Saxophoni, kwa kuwa kulikuwa na fununu kwamba wamejiunga na katika bendi ya Victoria Sound.


Baadhi ya wanamuziki wanaotajwa katika makala hii, wamekwisha tangulia mbele za mungu akiwemo Mzee Muhidini Gurumo. Wengine ni TX Moshi William, Nicko Zengekala, Selemani Mbwembwe, Joseph Maina, Mustafa John Ngosha, Suleimani Mwanyiro, Tino Maselenge ‘Arawa’,  Athuman Momba na mpulizaji wa saxophoni Alli Rashidi aliyefariki dunia siku ambayo bendi hiyo ikitimiza miaka 50, Oktoba 10, 2014.

Mwisho.

No comments: