Sunday, March 10, 2013

MIRIAM MAKEBA 'MAMA AFRIKA'










MIRIAM MAKEBA ‘Mama Afrika’

 
Novemba 05, 2012.

Laiti kama angelikuwa hai Miriam Makeba ‘ Mama Afrika’  Ijumaa iliyopita Novemba 09, 2012, tungelisherehekea miaka 80 ya kuzaliwa kwake. Lakini kwa masikitiko makubwa siku hiyo ndugu na wapenzi wa muziki wake duniani walikuwa katika maombolezo ya miaka minne tangu kifo chake.

Mwanamuziki Makeba alizaliwa Machi 04, 1932 huko Afrika ya Kusini na alifariki Novemba 09, 2008 akiwa na umri wa miaka 76.

Wazazi wake walikuwa Sangoma, Baba yake alikuwa mganga wa kienyeji toka Kabila la Xhosa.
Mama huyu Miriam  katika maisha yake amekumbana na matatizo mengi likiwemo lile la kukaa jela miezi Sita akiwa bado mchanga wa miezi sita akiambatana na mama yake mzazi aliyekuwa akitumikia kifungo.


Miriam ataendelea kukumbukwa kwa sauti  yenye mvuto wa aina yake ambayo yaelezwa kwamba haijawahi kusikika toka kwa mwanamuziki mwingine wa kike huko Afrika ya  Kusini.

Yaelezwa kwamba baada ya kutoweka kwa miongo mitatu akiwa nje ya nchi yake, Miriam Makeba siku aliyotua nchini humo alipokelewa na kufanyiwa sherehe kamambe iliyofananishwa mithiri ya sherehe ya malkia aliyerudi katika kiti chake.

Makeba alikuwa mwanzilishi wa nyimbo za kiafrika na alisaidia kuleta mageuzi  ya muziki wa kiafrika hadi akaitwa ‘Mama Afrika’ miaka ya 1960.

Kipaji chake kilianza kuonekana mwaka 1953  baada ya kuimba wimbo wake wa kwanza wa 'Laktshona Liange’. Wimbo huo  ulibeba  ujumbe mzito akiwa katika kundi  la akina Kaka la Manhattan Brothers.

Makeba aliachana na kundi hilo na akaanzisha kundi la wanawake lilijulikana kama Skylarks. Lakini mwaka mwaka 1958 alirejea tena katika kundi la Manhattan baada ya wao kukubali kazi ya mwanamke katika muziki.

Mwaka 1959 alianza ziara ya miezi 18 akizunguka nchini Afrika Kusini akishirikiana na bendi ya Aifherbert’s Musical Extravaganza African Jazz.

Miriam alitengeneza video yake ya kwanza inayoitwa Come back Africa ambayo ilimletea  mafanikio makubwa ya kupata mialiko mingi ya kwenda kuimba nchi za Ulaya na Marekani.

Akiwa Marekani Makeba aliifurahisha jamii ya Wamerekani weusi kwa wimbo wake wa ‘Pata Pata’ uliokuwa ndiyo Nembo yake.

Wimbo huo uliandikwa na Dorothy Masuka na kurekodiwa nchini Afrika ya Kusini mwaka 1956, kabla ya kuanza kuwa rekodi kali huko Marekani mwaka 1967.

Mwishoni mwa mwaka 1959, Makeba alifanya maonyesho kwa wiki nne mfululizo katika kijiji cha Vanguard huko New York, nchini Marekani.  

Umaarufu wake uliongezeka maradufu baada ya kufanywa kuwa mgeni maalumu wakati wa  tamasha la mwanamuziki Harry Belafonte katika ukumbi wa Carnegie, nchini Marekani.

Mwaka 1960 alifayatua album mbili kali ambazo zilimletea tuzo ya heshima ya Grammy.  

Makeba aliingia mkataba wa kushirikiana na mwanamuziki Harry Belafonte, ambapo mwaka 1972 walitoa Album iliyokuwa na jina la Belafonte & Miriam Makeba.

Miriam kwa mara nyingine tena mwaka 1997 alifanywa mgeni rasmi kwenye onyesho la Harry Belafonte Tribute kwenye bustani ya Madison Square.

Nyimbo zake alizotunga za kutangaza kupinga vita dhidi ya ubaguzi wa rangi, zilimletea mafanikio makubwa mwaka 1960.

Baada ya miaka 30 Makeba alilazimishwa kuwa raia wa Ulimwengu baada ya kutunukiwa zawadi ya Amani ya  Dag Hammarskjöld mwaka 1968.

‘Ndoa ndoana’ usemi ulijionyesha wazi kwa Makeba baada ya kuolewa na mwanaharakati mweusi Stokely Carmichael. Matamsha mengi yalifutwa pia mkataba wake wa kurekodi RCA ukafutwa. Matokeo yake ilikuwa matatizo makubwa yakamkumba  msanii huyu.

Rais wa Guinea wakati huo, Sekou Toure  alimwalika nchini mwake, naye akakubali na  akafanywa kuwa mmoja wa wanamsafara wa Guinea kwenda Umoja wa Mataifa.

Miaka ya 1964 na 1975 Mama Afrika Makeba alihutubia mkutano mkuu wa Umoja wa Mataifa, kuhusu ubaguzi wa rangi huko New York nchini Marekani.

Mwaka 1988 Makeba aliandaika wasifu wake ulioitwa Miriam: My Story, kwa lugha ya Kiingereza. Baadaye wasifu huo ulitafsiriwa na kuchapishwa katika lugha za Kijerumani, Kifaransa, Kitaliani Kiispaniola na Kijapani.

Kufuatika kuachiwa huru kwa  Nelson Mandela ‘mzee Madiba’ toka gerezani, Makeba alirudi nchini mwake Afrika ya Kusini mwezi Desemba 1990.

Alifanya onyesho lake la kwanza chini humo mwezi Aprili 1991 baada ya kutoweka kwa  miaka 30 akiwa nje ya nchi yake.

Alitunukiwa tuzo ya ushindi kwa wimbo wa  Sarafina mwaka 1992. Kwenye wimbo huo Makeba alicheza kama mama wa Sarafina.

Baada ya miaka miwili alirudiana na mume wake wa kwanza mpulizaji wa Trumpeti Hugh Masekela.

 Mwaka 1995 Makeba aliunda taasisi isiyo ya kiserikali (NGO) ya  kutunisha mfuko wa kusaidia na kulinda haki za wanawake wa Afrika ya Kusini.

Mwaka huohuo alifanya tamasha kubwa kwenye ukumbi wa huko Vatican's Nevi wakati wa sikukuu ya Krismasi.


Mungu aiweke roho yake pahala pema peponi, Amina.

 Mwisho.


No comments: