Sunday, March 10, 2013

SAMBA MAPANGALA ‘ANAYE VUNJA MIFUPA MAREKANI’



SAMBA MAPANGALA ANAYE VUNJA MIFUPA MAREKANI


SAMBA MAPANGALA ni mtunzi na mwimbaji maarufu wa kimataifa aliyejizolea sifa tele   Afrika ya Mashariki na Kati hususani katika nyimbo zake za ‘Vunja Mifupa’ na ‘Dunia tunapita’

Ni mwanamuziki mwenye kipaji cha aina yake, anaye kula ‘Kuku’ katika jiji la Washington DC nchini Marekani. Alimfanyia kampeni rais Barack Obama wa Marekani mwaka 2008.

Alizaliwa huko  Matadi  katika  mkoa uliojulikana  kama Bas-Congo huko Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo. Miaka ya 1970 alipiga muziki na bendi nyingi katika jiji la Kinshasa wakati akiwa katika masomo ya Sekondari.

Kipaji cha Mapangala kigundulika kupitia  tungo zake ambazo kila wimbo una ujumbe mzito masikioni mwa msikilizaji. Mfano wa karibu ni wimbo wa ‘ Dunia tunapita’ Wimbo huu unaelezea juu ya jamaa ambaye hawezi kufanya chochote kile bila kupita kwa waganga.

Kunyooka kwa Safari ya Samba Mapangala  katika masuala ya muziki kulianza kuonekana  mapema miaka ya 1970 alipoondoka Matadi kwenda katika Jiji la Kinshasha kwa ajili ya masomo ya Sekondari.

Sifa kubwa aliyonayo  Mapangala ni ya kuweza  kutunga, kuimba nyimbo kwa lugha za Lingala na Kiswahili  pia uwezo mkubwa alionao wa kumiliki Jukwaa.

‘Kizuri chajiuza kibaya chajitembeza’ Usemi huu ulijidhihirisha kwa Mapangala baada ya kuonyesha umahiri mkubwa kupitia sauti yake nyororo kulipelekea kupata kazi ya kupiga muziki kwenye bendi za Bariza, Super Tukina, Bella Bella na Saka Saka katika jiji la Kinsahasa huko Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo.


Juhudi zake katika muziki zilimfikisha kusafiri na wanamuziki wenzake kwenda  Mashariki mwa Kongo mwaka 1975. Mwaka iliofuatia wa 1976 walivuka mpaka kwenda Kampala nchini Uganda hako wakaunda bendi ya Le Kinois.

 Akiwa mwimbaji Kiongozi Samba Mapangala  na bendi yake ya Les Kinois ilihamisha makazi toka Kampala na kwenda jiji la Nairobi nchini  Kenya mwaka 1977.

Licha ya kuwa na ushindani mkali toka bendi zingine kubwa katika jiji katika hilo la Nairobi, bado Les Kinois walifanikiwa kuliteka jiji hilo kwa kasi kubwa.

Wakati huo jiji la Nairobi kulikuwa na bendi za Super Mazembe, Orchestra  Les Mangelepa, Les Wanyika, Orchestra Moja One , Baba Gaston  na nyingine nyingi.

Ili kuonyesha ukomavu katika muziki, Samba aliamua kujitegemea mwenyewe kwa kuunda bendi yake na kuipa jina la Orchestra Virunga mwaka 1981 bendi ambayo kwa kipindi kifupi  ikakubalika na wapenzi wa muziki na kuwa moja kati ya bendi maarufu Afrika Mashariki.

Samba Mapangala hupiga muziki wake ukiwa na mchanganyiko wa staili za rumba na Soukous kutoka Kongo. Ili kuwaridhisha wapenzi wa muziki wa Nairobi na vitongoji vyake  walipiga muziki kwa staili za watu wa Kenya.

Rekodi ya kwanza ya Virunga  iliyoitwa ‘It's Disco Time with’  ilitoka mwaka 1982.

Mapangala na bendi yake ya  Virunga walisafiri kwenda  nchini Uingereza  mwezi Aprili  1991 na huko walifanya maonyesho makubwa takribani 23.

Baada ya kufurahia mafanikio ya safari yao, walifanya safari nyingine ya mwisho mwaka 1997 wakipitia nchi za Afrika hadi Marekani ya Kaskazini.

Album za Samba Mapangala  zilizopo ni pamoja na Virunga Volcano  ya mwaka 1990, Evasion ya  1983, Feet on Fireya ya 1991, na  Karibu Kenya iliyofyatuliwa mwaka 1995 zilizorekodiwa katika jiji la  Paris  nchini Ufaransa  akiwashirikishwa wanamuziki toka bendi  ya  Les Quarters Etoiles na  wanamuziki wengine nguli waliokuwa hapo Paris.

Album ya  Vunja Mifupa  iliyotoka mwaka 1997  ilichukua soko kubwa la mauzo hususani Afrika ya Mashariki ikizingatiwa  Ujumbe unatolewa kwa lugha ya Kiswahili.
Virunga Roots Volume 1,  ulijumisha nyimbo zilizo katika kumbukumbu  Virunga  na kutolewa mwaka 2005.

Samba kwa kawaida ni mpole na mcheshi, mwaka   2000,  alialikwa kwenye  Sherehe ya siku ya Jamhuri ya watu wa Kenya katika jiji la London,  ambapo muziki waliopiga ‘uliwachengua’ watu  wote waliofika katika sherehe hiyo.

Mzee wa ‘Vunja Mifupa’ Samba Mapangala  alikuja Tanzania mwezi Mei 2004 kwa ziara ya wiki mbili  na kufanya  maonyesho kadhaa.

Nguli huyu hupenda kushirikina na wanamuziki wengine ili kubadilishana ujuzi na uzoefu. Aliwahi kupiga muziki akiwa na safu ya wanamuziki nyota toka nchi za Kenya na Tanzania.

Album yake mpya ya Song and Dance iliyorekodiwa mwaka 2006 katika Studio za Virunga reocords, wakimshirikisha mwanamuziki  
Bopol na wangine wakali  toka bendi yake ya Orchestra Virunga. Abum hiyo iliyokuwa  na nyimbo nyingi ilizinduliwa rasmi walipokuwa kwenye ziara nchi za Ulaya mwezi March 2006.

Mwezi Juni 4 2006 Samba alikuwa nchini Kenya  kawa ajili  shughuli maalumu ya  Ecofest,

Wakati wa Kampeni ya Urais wa Marekani mwaka 2008, Samba Mapangala alionyesha ni jinsi gani wananchi wa Kenya wanavyomshabikia mgombea wa kiti hicho Barack Obama. Alifyatua wimbo maalumu wa kumtakia heri Obama ulioitwa '
Obama Ubarikiwe'

SambaMapangala na bendi yake ya Orchestra Virunga walirejea Afrika ya Mashariki mapema mwaka 2009, na kutoa burudani katika jiji la Nairobi na  Zanzibar ambako alialikwa katika tamasha la Sauti za Busara .

Mwishioni mwa mwaka 2009 Samba aliuongezea nguvu mfuko wa World Wildlife Fund  kwa kutunga na kutoa  bure  wimbo  wa ‘ Mlima wa Magorila’ uliokuwa ukitoa wito kusaidia kuwalinda magorila waliopo katika Hifadhi ya Taifa ya Wanyamapori ya Virunga ya nchini Kenya ambako wanyama hao adimu hupatikana.
Mangwana anakumbukwa na wapenzi wa muziki wa dansi katika nchi za Afrika ya mashariki na Kati pale wasikiapo nyimbo za Hadija, Marina Nyama Choma,  Alimasi, Dunia haina mwisho na  Dunia tunapita. Nyingine ni  Jaffar, Mapenzi hayana macho, Muniache, Virunga, Vijana, Ufunguo, Vunja mifupa, Siri na Vidonge  uliopigwa kwa staili ya mduwara. Nyimbo zote  zimeimbwa kwa lugha ya Kiswahili.
Samba Mapangala na familia yake wanaishi katika jiji la Washington DC nchini  Marekani.

Mwisho.


No comments: