Tuesday, May 12, 2015

ZAIKO LANGA LANGA KISIMA CHA MUZIKI


ZAIKO LANGA LANGA KISIMA CHA MUZIKI
 
Natumaini sitakosea kusema kwamba bendi ya Zaiko Langa langa ndiyo iliyoasisi takribani bendi nyingi za Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo.
Bendi hizo kama si zote zinazotamba nchini humo kwa sasa, ziliasisiwa na wanamuziki ama waliotoka ndani ya bendi hii au katika bendi zilizoanzishwa na wakali waliopata kuipigia.

Zaiko Langa Langa ni bendi kongwe huko Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo kwa sasa, ambayo bado inaendelea kudunda licha ya wimbi kubwa la kuhamwa na wanamuziki mahiri pamoja na ushindani uliopo hivi sasa.
Kimsingi haitakuwa vibaya kuitaja Zaiko Langa Langa kuwa ni chuo cha muziki nchini humo.
Sababu kubwa ni kwamba bendi nyingi zinazotamba hivi sasa, ambazo zimeanzishwa kuanzia miaka ile ya 1970, ni matunda yake.
Kwa upande wa wanamuziki nyota wa Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo akina Papa Wemba, Bozi Boziana, Dindo Yogo, Evoloko Ley Ley ‘Joker’, Defao Matumona, Koffi Olomide na wengine wengi, lazima utapata chimbuko lao kutoka kwenye shina la Zaiko Langa Langa.
Zaiko Langa Langa mpaka sasa bado ingali inaongozwa na mkongwe N’Yoka Longo Mvula.

Bendi nyingi za Isifi Lokole, Yoka Lokole, Viva la Musica, Langa Langa Stars, Zaiko Familia Dei, Choc Stars, Le Anti Choc, Le Grand Zaiko Wawa, Quartie Latin na nyinginezo nyingi, zimetoka kwenye chimbuko la Zaiko. Kwa sasa inajulikana kama Zaiko Langa Langa Nkolo Mboka, yaani ‘Wakuu wa Mji’.
Siyo ajabu kuona leo hii kuna idadi kubwa ya bendi zilizotokea ubavuni mwa Zaiko Langa Langa zikijiita ‘Ukoo wa Langa Langa’ (Clan Langa Langa).
Bendi hizo ni Isifi Lokole iliyoanzishwa na Papa Wemba, Bozi Boziana, Evoloko Jocker na Mavuela Somo. Yoka Lokole iliyoanzishwa na Papa Wemba, Bozi Boziana na Mavuela Somo. Grand Zaïko Wa Wa iliyoanzishwa na Felix ‘Pepe’ Manuaku Waku aliyeungana na Shimita El Diego na Djo Poster.
Halikadhalika kwa bendi ya Viva La Musica iliyoanzishwa na Papa Wemba akiwa na Emeneya Mubiala na Theodore Djangi Dindo Yogo.
Choc Stars iliyoanzishwa na Bozi Boziana, Tshimpaka Roxy na kuungana na akina Ben Nyamabo, Carlito Lassa, na Defao Matumona. Bendi ya L'Orchestre Anti-Choc iliyoanzishwa na Bozi Boziana akiungana na Deyesse Mukangi, Jolie Detta, Dodoli, Walingonda, Fifi Mofude na wengineo.
Bendi ya Langa Langa Stars iliyoanzishwa na Verckys Kiamuangana Mateta, Evoloko Jocker, Bozi Boziana, Tshimpaka Roxy, Emeneya Mabiala na Djo Mali.
Zaiko Langa Langa Familia Dei ya Lengi Lenga, Ilo Pablo, Bimi Ombale, Beniko Popolipo, Petit Poisson, na Djimi Yaba.
Zaïko Langa Langa Nkolo Mboka yenyewe chini ya N'Yoka Longo, Meridjo, Oncle Bapius, Zamuangana, Nono Atalaku, Mbuta Matima, Malage de Lugendo, Adamo Ekula, Baroza na Shiro Shiro.
Zaiko Universel ya Meridjo na Oncle Bapius Muaka. Langa Langa Rénové ya Evoloko Jocker. Basilique Loningisa iliyoanzishwa na Bimi Ombale.
Etumba na Ngwaka Aye ilikuwa chini ya marehemu Dindo Yogo. Les Quatros de Langa Langa ukiwa ni muungano wa Papa Wemba, Evoloko, Bozi Boziana na Gina Efonge.
Les Stars de Zaiko (sasa inaitwa Zaikas Kolo Mboka) ikiwa chini ya Adamo Ekula, Petit Poisson, Tshanda na Papy Cocaine; na Clan Petrole ambapo nyimbo nyingi zimerekodiwa kupitia majina ya makundi tajwa hapo juu yanayowakilisha Ukoo wa Langa Langa.



Historia ya kuzaliwa kwa Zaiko Langa Langa imekuwa ikikosewa sana na baadhi ya watu wakidai kwamba ilianzishwa mwaka 1970.
Taarifa hiyo ni potofu kwa kuwa ilianzishwa rasmi Desemba 24, 1969 jijini Kinshasa, Jamhuri ya Kidemokrasi ya Kongo, ikijulikana kama Orchestra Zaiko.
Kwa mamneno ya mafupi ya lugha ya  Lingala ya Zaire ya bankoko (Zaire ya babu zetu).
Neno Langa Langa lina utata kidogo amapo kwenye ‘wavuti’ ya bendi linamaanisha ‘Utukufu’, lakini kwa mujibu wa kiongozi wa bendi hiyo N’yoka Longo alisema kuwa maana ya Langa Langa ni ‘Maji Maji’ (kwa maana nyingine walichukua jina la Mto Kongo).
Hivyo kirefu chake ama tafsiri yake halisi ni Kongo ya mababu zetu ni ya maji maji.
Wakati huo muziki toka Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo ulitawaliwa zaidi na bendi za African Jazz ya Joseph Athanase Tchamala Kabasele ‘Le Grand Kalle’, African Fiesta ya Nicolas Kassanda wa Mikalay maarufu kama Dk. Nico Kasanda na Tout Puisant Orchestre Kinnie Jazz (TP OK Jazz) ya L’Okanga La Ndju Pene Luambo Luanzo Makiadi Franco. Hata African Fiesta National ya Pascal-Emmanuel Sinamoyi Tabu, almaarufu Tabu-Rey Rochereau, aliyoianzisha baada ya kutengana na Dk. Nico na mwaka 1970 akaibadili jina na kuiita Orchestre Afrisa Intanatinale.
Waanzilishi wa Zaiko Langa Langa walikuwa wanamuziki ambao baadhi walikuwa wanapigia bendi ndogo ndogo tu za mitaani na wengine walikuwa wanafunzi. Hawa si wengine bali ni mpiga konga maarufu D.V. Moanda, ambaye jina lake halisi ni Vital Moanda-di Veta, Marcelin Delo, Henry Mongombe, Olemi Eshar-Eshar dem’belinana Andre Bita.
Wengine ni Mavuela ‘Somo’ Simeon, Evoloko Lay Lay ‘Joker’, Teddy Sukami, Oncle Bapius aliyekuwa akipiga gitaa la besi, Zamuangana Enock le meilleur, baba ya wapiga solo wa kizazi kipya Congo Felix Manuaku Waku (pia alijulikana zaidi kama Pépé Fely), na N'Yoka Longo Mvula, anayelikana kama Jossart, ama Vieux Mbombas, lakini maarufu zaidi kama N’Yoka Longo, aliye na asili toka nchini Angola.
Hawa walikuwa wakipiga muziki wa soukous. Kwa upande wa Pop, muziki uliokuwa ukifungua pazia katika shoo zote za bendi hiyo, kulikuwa na Bimi Ombale, Mbuta Matima Zephirin na Mashakado Mbuta. Wengine walikuwa ni Moanda, Mongombe, Marcelin, Waku, N’Yoka Longo na Andre Bita walitokea kwenye bendi ya mtaani iliyojulikana kama Bel Guide National. Wote hawa walikuwa wanafunzi wakitokea katika familia za matajiri jijini Kinshasa.

Baadaye mwaka huo bendi hiyo ikamchukua bwana mdogo mwenye miaka 19, ambaye alikuwa anaimba kwaya kanisani. Huyu si mwingine bali ni Jules Shungu Wembadia Pene Kikumba, maarufu kama Papa Wemba.
Mwisho.

No comments: